Habari

AHADI HEWA! Ndoto za Boma Yangu zakwama

Na PATRICK ALUSHULA April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAKRIBAN asilimia 80 ya Wakenya waliojisajili katika mpango wa nyumba za bei nafuu hawajawahi kuweka akiba yoyote kufikia kiwango cha chini kinachohitajika ili kuhitimu kutengewa nyumba, hali inayozua maswali kuhusu uhalisia wa utekelezaji wa mpango huo.
Hatua hii inaonyesha ni vigumu kwa watu hao kutimiza ndoto zao za kumiliki nyumba kupitia mpango huo wa serikali.
Takwimu za hivi punde zinaonyesha kuwa asilimia 79.97, sawa na watu 816,780 kati ya waliojisajili kwenye jukwaa la Boma Yangu linalowezesha Wakenya kuweka akiba, kuchagua na kuhifadhi nyumba wanazotaka hawajatoa mchango wowote.
Kufikia mwisho wa Mei 2025, Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) lilisema ni watu 163,598 pekee, sawa na asilimia 20.03 ya wanachama wote, waliokuwa wameanza kuweka akiba kuelekea kupata nyumba.
Kwa mujibu wa masharti ya mpango huo, waombaji wanapaswa kujisajili kwenye mfumo wa Boma Yangu kisha waanze kuweka akiba hadi wafikie angalau asilimia tano ya thamani ya nyumba wanayolenga.
Ni baada ya kufikia kiwango hicho ndipo wanapoweza kuzingatiwa kwa mgao wa nyumba.
Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kuwa hata miongoni mwa walioanza kuweka akiba, wengi bado wako mbali na kufikia kiwango hicho.
NHC ilibainisha kuwa asilimia 98.13 ya wachangiaji, sawa na watu 160,534, walikuwa wameweka chini ya Sh100,000 kufikia Juni 2025.
Watu 46 pekee ndio waliokuwa wameweka zaidi ya Sh1 milioni, idadi ndogo sana ikilinganishwa na mahitaji ya soko.
Mpango wa ujenzi wa nyumba nafuu unafadhiliwa kupitia ushuru wa asilimia 1.5 unaokata mshahara kwa mfanyakazi, huku waajiri wakichangia kiwango sawa kila mwezi.
Hata hivyo, licha ya makato haya ya lazima, waombaji bado wanahitajika kuweka akiba ya hiari ya asilimia tano ya thamani ya nyumba kabla ya kutengewa wanazotaka. Baada ya hapo, wanapaswa kuendelea kulipa hadi wamiliki nyumba kikamilifu.
Bodi ya Nyumba Nafuu ilisema kuwa jumla ya Sh125 bilioni zimekusanywa kupitia Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA) tangu kuanzishwa kwa ushuru huo, huku Sh73.1 bilioni zikikusanywa katika mwaka uliomalizika Juni 2025 pekee.
Ushuru huo ulioanzishwa Machi 2024 umekuwa ukizua mjadala mkali, huku wafanyakazi na waajiri wakitoa maoni tofauti kuhusu ufanisi wake.
Aina ya nyumba inayopatikana inategemea kiwango cha mapato ya mwombaji.
Wanaopata hadi Sh19,999 kwa mwezi huangukia katika kundi la nyumba za kijamii, wale wanaopata kati ya Sh20,000 na Sh149,999 hupewa nafasi katika nyumba nafuu, huku wanaopata zaidi ya Sh150,000 wakilengwa kwa nyumba za tabaka la kati.
Kwa mujibu wa NHC, thamani ya hazina ya nyumba ilikuwa Sh1.08 bilioni kufikia Mei 2025, huku kukiwa na ongezeko la asilimia 41 ya waliojisajili na asilimia 93 ya wanaochangia.
Kati ya fedha hizo, Sh764.2 milioni ni akiba ya wanachama ambao bado hawajatengewa nyumba, huku Sh320.7 milioni zikiwa mapato yaliyopatikana kupitia uwekezaji.
Sehemu kubwa ya fedha hizi imewekezwa katika hati za dhamana za muda mfupi za serikali, huku kiasi kingine kikiwa katika akaunti za fedha taslimu, hatua ambayo mamlaka husika inasema inalenga kulinda na kukuza thamani ya fedha kabla ya kutumika kwenye miradi ya ujenzi.
Tangu kuanzishwa kwa mpango huo, wanachama 597 wa Boma Yangu wamefanikiwa kuwa wamiliki wa nyumba kupitia mradi wa Park Road, uliokuwa wa kwanza kukamilika.
Kwa sasa, jumla ya nyumba 210,446 zinaendelea kujengwa katika maeneo mbalimbali nchini na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2026.
Hata hivyo, changamoto kuu inasalia kuwa kiwango kidogo cha wananchi kuweka akiba, hali inayoweza kudhoofisha lengo la mpango huo wa kuhakikisha Wakenya wengi wanapata makazi bora kwa gharama nafuu.
Wataalamu wanasema bila kuongeza uhamasishaji na kuweka motisha zaidi kwa wananchi kuweka akiba, mpango huo unaweza kukumbwa na vikwazo vikubwa katika kufikia malengo yake ya muda mrefu.