Habari

Nenda ushtaki kwa polisi, Duale aambia Mbunge aliyedai kudhulumiwa na hospitali

Na EDWIN MUTAI February 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Afya Aden Duale amemtaka Mbunge wa Mosop Abraham Kirwa awasilishe rasmi malalamishi dhidi ya Nairobi Hospital na daktari aliyemtibu na kusababisha apate kiharusi.

Ugonjwa huo ulimsukuma asake matibabu nje ya nchi na akakosa kuhudhuria vikao vya bunge na umma kwa kipindi cha miaka miwili.

Bw Duale alisema sheria inamruhusu Bw Kirwa kuwasilisha malalamishi ya utepetevu dhidi ya hospitali na daktari aliyemtibu.

“Natumai umewasilisha malalamishi kwa Baraza la Muungano wa Wahudumu wa Kimatibabu na Matabibu Nchini (KMPDC) kwa sababu kile kilichofanyika hakikubaliki kamwe,” akasema Bw Duale.

“Shida ni daktari ambaye hakukupa dawa zilizofaa na hafai kuachwa hivyo kwa sababu Wakenya wengi wamepoteza maisha kutokana na utepetevu kama huo,” akasema.

Waziri alisema hayo wakati wa Kongamano la Wabunge Naivasha Jumatano. Bw Kirwa alisema alikuwa amezungumza na wakili wake wafuatilie suala hilo na KMPDC.

“Sijawasilisha malalamishi na KMPDC lakini nitaamrisha wakili wangu afanye hivyo. Kile ambacho daktari na Hospitali ya Nairobi walinifanyia hakikubaliki,” akasema Bw Kirwa kwenye mahojiano na Taifa Leo baada ya mkutano huo.

“Mbona niteseke kwa sababu ya utepetevu wao? Wakenya wangapi wanakufa kwa sababu ya utepetevu wa madaktari ? Kama hili linaweza kufanyikia mbunge itakuaje kwa Mkenya wa kawaida?” akauliza.

Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangúla alisimulia kisa cha kibinafsi ambapo mjomba wake aliaga dunia akitibiwa na daktari miaka miwili iliyopita.

Alisema kuwa utepetevu huo wa madaktari mara nyingi hufanywa na wataalamu ambao katika baadhi ya matukio huwa wanawakinga wenzao.

“Mjombangu alienda kwa daktari mtaalamu ambaye alikuwa amelewa na akamtibu kwa sumu na akafa papo hapo. Tuna matukio kama hayo na namwomba mwenyekiti wa kamati ya afya Dkt James Nyikal ahakikishe visa kama hivi vinachunguzwa na madaktari kama hawa wanachukuliwa hatua za kinidhamu,” akasema Bw Wetangúla.

Bw Duale alifichua kuwa tabibu feki hivi majuzi alisababisha mauti ya mgonjwa akimngóa meno na ikabainika hakuwa Mkenya wala hakuwa amesajiliwa na KMPDC.

“Hajawahi kuenda chuo cha kimatibabu. Katika Kaunti ya Tharaka Nithi, tuliambiwa kuna raia wa Nigeria ambaye wagonjwa wake walikuwa wanawake na walikuwa wakifa sana,” akasema Bw Duale.

Waziri huyo alikiri kwamba ufisadi umekita mizizi katika Bodi ya Famasia na Sumu Nchini lakini akasema kumekuwa na mageuzi kwenye taasisi hiyo.

“KMPDC ilikuwa ikitumika kutoa leseni kwa yeyote ambaye alikuwa akilipa. Mwanzoni nilikuwa nikikataa kuwa ufisadi ulikuwa umepiga kambi katika jumba la Afya lakini wiki mbili baada ya kuingia humo, nikabaini ni kweli,” akasema.