Ni maafa tu ajali mbaya barabarani Webuye ikiongeza huzuni ya mafuriko yaliyoua 49
MAAFA yanaendelea kushuhudiwa nchini huku watu 15 wakifariki kwenye ajali ya barabara na idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko ikiongezeka hadi 49.
Vifo kutokana na ajali barabarani vimeongeza huzuni nchini baada ya watu 15 kufariki dunia katika ajali iliyotokea katika makutano ya Malaha kando ya barabara kuu ya Webuye-Kitale katika Kaunti ya Bungoma.
Ajali hiyo ilitokea Jumatatu usiku baada ya lori linalodaiwa kupoteza mwelekeo kugonga magari kadhaa ikiwemo matatu ya abiria na pikipiki, na kusababisha magari kadhaa kugongana.
Walioshuhudia walisema lori hilo lilipoteza mwelekeo kabla ya kuligonga gari la abiria na pikipiki zilizokuwa karibu na makutano hayo yenye shughuli nyingi.
Simanzi imetanda katika kijiji cha Malaha, Webuye baada ya ajali hiyo kuua watu 15 na kuwaacha wakazi wakiduwaa.
Miongoni mwa waliopoteza maisha ni watu sita wa familia moja na wengine watatu wa familia nyingine, hali iliyoongeza maumivu kwa jamaa zao.
Katika boma la Bw Ezekiel Kinusu, huzuni imetanda baada ya ajali hiyo kuangamiza jamaa sita wa familia yake, akiwemo mamake, ndugu zake watatu na jamaa wengine wawili.
Bw Kinusu alisema waathiriwa hao walikuwa wameungana na wakazi wengine waliokusanyika barabarani baada ya waendesha pikipiki wawili kuhusika katika ajali ya awali.
Dakika chache baadaye, lori lililokuwa likitoka upande wa Lugulu kuelekea Webuye lilipoteza mwelekeo na kukanyaga watu katika umati huo.
“Tumepoteza karibu familia nzima. Huu ni uchungu ambao ni vigumu kueleza,” alisema akiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti Ndogo ya Webuye huku akijaribu kukubali uzito wa msiba huo.
Aliongeza kuwa lori hilo lilitoka barabarani hadi walikokuwa watu, huku baadhi yao wakisukumwa hadi mtoni.
“Hata tulisaidia kutoa miili ya baadhi ya waathiriwa kutoka mtoni,” alisema kwa sauti ya huzuni.
Kutokana na mkasa huo, familia kadhaa sasa zinakabiliwa na jukumu gumu la kupanga mazishi ya watu wengi kwa wakati mmoja huku zikipambana na majeraha ya kihisia.
Polisi wamethibitisha kuwa idadi ya waliofariki imefikia 15. Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Webuye Rosemary Odeke alisema watu 10 walifariki papo hapo huku wengine wakifariki wakipokea matibabu hospitalini.
Miili ya waathiriwa imehifadhiwa katika mochari ya Hospitali ya Rufaa ya Kaunti Ndogo ya Webuye huku familia zikianza maandalizi ya mazishi.
Maafa yaliyotokana na mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi nayo yanazidi
Kwa mujibu wa taarifa ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS), idadi ya watu waliofariki dunia kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa imefikia 49 kote nchini.
Maelfu ya familia pia zimeathiriwa vibaya baada ya maji ya mafuriko kusomba nyumba, barabara na mali nyingine muhimu.
Polisi walisema takriban familia 2,624 zimelazimika kuhama makazi yao baada ya nyumba zao kufunikwa na maji.
Aidha, miundombinu kama barabara, daraja na majengo imeharibiwa vibaya katika maeneo mbalimbali.
Katika taarifa hiyo, NPS ilisema inaomboleza pamoja na familia zilizopoteza wapendwa wao katika janga hilo.
Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja pia alieleza kuwa licha ya changamoto zinazosababishwa na mafuriko, maafisa wa polisi wanaendelea kutoa huduma za usalama kwa wananchi.
Polisi walisema angalau vituo 16 vya polisi vimeathiriwa na mafuriko, jambo linalosababisha changamoto katika utoaji wa huduma za usalama katika maeneo yaliyoathiriwa.
Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya limesema idadi ya walioathiriwa inaweza kuwa kubwa zaidi.
Shirika hilo linaeleza kuwa watu 4,845 wamelazimika kuhama makazi yao huku familia nyingi zikikimbilia maeneo ya juu ili kujinusuru na maji ya mafuriko.
Mbali na kuharibu makazi ya watu, mafuriko pia yameharibu zaidi ya ekari 20,800 za mashamba, hali inayotishia usalama wa chakula ikiwa mvua itaendelea kwa muda mrefu.
Wakati huo huo, Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa Kenya imeonya kuwa mvua itaendelea kunyesha katika maeneo sita nchini ikiwemo Magharibi mwa Kenya, Nyanda za Juu za Kati, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa, maeneo ya chini ya Kusini Mashariki na Pwani ya Kusini.
Hata hivyo, wataalamu wa hali ya hewa wamesema nguvu ya mvua inaanza kupungua kidogo, hali inayotoa matumaini kwa wananchi walioathiriwa na mafuriko.