Habari

Nilifuatiliwa kwa wiki moja kabla ya kukamatwa, asema Njeri

Na KEVIN CHERUIYOT June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

ROSE Njeri, mwanaharakati ambaye alikamatwa na maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) hivi majuzi kwa dai alivuruga barua pepe ya kamati ya bunge, amesimulia jinsi polisi walivyomfuatilia kwa zaidi ya wiki moja kabla ya kumkamata Ijumaa, Mei 30.

Siku hiyo, Rose alikuwa ameamka kwenda kuhudhuria mahafali baada ya kukamilisha kozi ya miezi miwili ya uboreshaji wa taaluma katika teknolojia ya habari (IT).

Baada ya hafla ya mahafali, alipokuwa akipiga picha na marafiki wake, mwanamke asiyejulikana alimtaka aandamane naye nje ya jengo.

Alitilia shaka nia ya mwanamke huyo, aliyemshurutisha kuingia moja ya magari aina ya Subaru Forester yaliyokuwa yamesimama karibu, na ndani yake kulikuwa na maafisa wa DCI.

“Nilimuuliza alitaka nini na akaniambia twende tuongee nje. Nilipojaribu kukataa, alianza kunisukuma. Kulizuka mtafaruku na ghafla nikajikuta ndani ya gari, nikiwa katikati ya watu wawili nyuma na wengine wawili mbele,” alisema Bi Njeri katika mahojiano na Taifa Leo.

Ndipo alielezwa alikamatwa kwa sababu ya tovuti aliyotengeneza kuwapa Wakenya fursa ya kutoa maoni yao kuhusu Mswada wa Fedha wa 2025.

Rose anasema kuwa alijitolea kuunda tovuti hiyo baada ya kuona ombi kwenye mtandao wa X (Twitter) la kutafuta mtu wa kutengeneza jukwaa la kuwasilisha maoni kwa Kamati ya Fedha.

Tovuti hiyo ilikuwa na uwezo wa mtu kuandaa barua ya maoni ambayo mtumiaji angeweza kuhariri na kisha kuituma kupitia barua pepe kwa kamati husika.

Wiki moja kabla ya kukamatwa, alidai alipokea simu za ajabu na ujumbe kutoka kwa makampuni ya mikopo ya kidijitali ambayo hakuwahi kujisajili nayo.

“Nilipokea taarifa kuhusu programu ambazo hazikuwa kwenye simu yangu. Nilibadilisha laini lakini bado nilipokea simu za salamu za ajabu,” alieleza.