Habari

Nimekuja kuboresha NMG, asema Rostam Azizi baada ya kununua hisa za Aga Khan

Na FATUMA BARIKI March 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MMILIKI mpya mwenye hisa nyingi katika kampuni ya Nation Media Group, Bw Rostam Azizi amesema kwamba mkakati wake mkuu ni kuimarisha biashara na kuipanua zaidi kuongeza ajira.

Akizungumza katika kikao na wanahabari katika hoteli moja jijini Nairobi siku moja baada ya tangazo kwamba kampuni yake, Taarifa Limited imenunua asilimia 100 ya hisa za shirika la Aga Khan katika NMG, Bw Azizi alisema nia yake kuu katika kutwaa biashara hii ni kuendeleza uanahabari usioegemea upande wowote ambao umekuwa ukiendelezwa na Muadhama The Aga Khan tangu kuasisi kampuni hiyo miaka 66 iliyopita.

Alisema mchango mkubwa atakaofanya ni kuongeza uwekezaji ili kuhakikisha huduma za kampuni zinafikia sehemu kubwa zaidi ya umma na haswa vijana ili kuiweka thabiti na kuvutia matangazo biashara miongoni mwa mbinu zingine zitakazozaa faida katika miaka ijayo.

SOMA PIA: Kampuni ya Aga Khan yauza hisa zake za Nation Media Group kwa Taarifa Limited ya Tanzania

Akipokea maswali kutoka kwa wanahabari, Bw Azizi alisema rekodi yake inaonyesha biashara zake ni za kipindi kirefu, kwa maana hiyo, akataka wafanyakazi wa NMG kuwa na imani kwamba amekuja kukaa muda mrefu, sio mwaka mmoja au miwili.

“Nia yetu si kupunguza ajira bali kuziongeza na kukuza kampuni. Nataka kuambia wafanyakazi wa Nation Media Group kwamba ari yetu ni kupanua biashara, sio kuipunguza. Tutabuni ajira zaidi, sio kuzipunguza,” akasema.

Kuhusu gazeti la Taifa Leo, Bw Azizi ambaye ndiye mmiliki wa kampuni ya Taifa Group ya Tanzania alisema ana habari kuhusu matatizo mbali mbali yanayoathiri ukuaji wake, akasema suluhisho atakalopendekeza ni mbinu za kibunifu za kuhakikisha gazeti hilo linasomwa kwingi zaidi ili kuongeza ukuaji wake.

“Kuna wakati ambapo mojawapo ya biashara zako zinashikiliwa na zile zinazofanya vizuri; ukiona gazeti linachechemea, unatakiwa kulibeba na kuenda nalo, sio kuliacha peke yake; tutakuwa wabunifu kuliimarisha,” akasema.

Bw Azizi alitetea pia ukaribu wake na Rais William Ruto ambao wachangiaji mitandaoni walikuwa wanaibua tetesi kuhusu ushirikiano wao hivyo kueleza hofu ya uanahabari wa NMG kuingiliwa kisiasa akisema Rais Ruto sio wa kwanza kwake yeye kuwa na urafiki; kwamba amekuwa na urafiki na viongozi wengi mashuhuri katika kanda ya Afrika Mashariki.

“Nilikuwa na ukaribu mkubwa zaidi na Raila; hata alikuwa mgeni mashuhuri harusi ya binti yangu; Ruto si wa kwanza kwangu kuwa na urafiki; dili ya Taifa Gas nilisaini na Uhuru,” akasema akisisitiza kwamba maono ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yatafaulu pekee kwa kujenga mahusiano baina ya mataifa hayo.