Habari

Sauti zaidi zajitokeza kuhoji mauaji ya Ojwang uongo wa polisi ukianikwa hadharani

Na DAN OGETTA, GEORGE ODIWOUR June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

RIPOTI ya upasuaji uliofanyiwa maiti ya mwalimu na mwanablogu, Albert Ojwang’ imebaini kwamba alipigwa vibaya kabla ya kufa, huku mwanapatholojia wa serikali akisema hakujiua kwa kujigonga ukutani polisi walivyodai.

Akiongea baada ya upasuaji wa mwili wa mwalimu huyo Jumanne Juni 10, 2025, katika Nairobi Funeral Home, Dkt Benard Midira alisema yeye na wanapatholojia waliowakilisha familia ya Ojwang na wadau wengine, walikubaliana kuwa kifo cha Ojwang kilisababishwa kwa kupigwa na watu wengine.

“Tulipata majeraha kwenye kichwa, dalili ya majeraha shingoni na sehemu zingine mwilini na miguuni,” akasema Dkt Midira.

“Majeraha hayo yanaonyesha kuwa alishambuliwa. Kulikuwa na dalili kwamba alipambana na washambuliaji wake akijaribu kujikinga,” akaongeza.

Dkt Midira aliongeza kuwa japo ni vigumu kubaini wakati ambapo alipata majeraha hayo, yalitokea ndani ya muda mfupi.

“Alivuja damu kwenye ubongo, alitokwa damu sehemu zingine za mwili. Hii inaonyesha kuwa hakujigonga,” akaongeza.

Rais wa Chama cha Wanasheria Nchini (LSK) Faith Odhiambo alielezea majeraha hayo kama yanayoonyesha kuwa Ojwang’ aliteswa kikatili, akisema wahusika walitekeleza mauaji ya kiholela.

“Kosa lake haitambuliwi na sheria. Kuna mtu aliyetoa amri Ojwang’ achukuliwe kutoka nyumbani kwao Homa Bay. Sharti mtu huyoi awajibike,” akasema Bi Odhiambo.

“Tutaendelea kuweka presha hadi maafisa wote waliohusika waadhibiwe kama watu binafsi. Sharti IPOA ichukue hatua, hatutakubali visingizio,” akaongeza.

Babake mwendazake Meshark Ojwang Opiyo, alielekeza lawama kwa mlalamishi Bw Eliud Lagat ambaye ni Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi (DIG)

“Ewe Eliud Lagat, je, ni wewe uliwatuma maafisa wako? Mbona uliua mtoto wangu. Alifanya kosa gani kupata adhabu kali kama hii? Mbona mtoto wangu alisalitiwa?”Mzee Opiyo akauliza.

“Hata ripoti ya polisi ilikuwa ya uongo. Ripoti ya upasuaji inaonyesha ukweli,” alisema na kumuomba Rais Ruto kuingilia kati.

“Nisaidie kama mlipa ushuru. Waliona boma yetu ni ya maskini na wakachukulia hatuna maana,” alisema.

Wakili aliyehudhuria upasuaji alihoji jinsi marehemu aliweza kuvua mavazi yake, ikiwemo fulana, ndani ya seli iliyofungwa, walivyodai polisi katika ripoti yao ya awali.

“Hii kesi inaibua maswali zaidi ya majibu. Naibu Inspkekta Jenerali wa polisi ametajwa kama mlalamishi lakini alipiga ripoti na kulalamika wapi na ni nani alitoa amri ya kukamatwa na kuteswa kwa marehemu,” aliuliza wakili Vincent Vusugwa.

Ojwang alikufa saa 24 baada ya kukamatwa, mwili wake ukiwa umevimba na kutokwa damu. Iliripotiwa na polisi kuwa alikuwa amejiua Nairobi, kilomita 320 kutoka nyumbani kwake kwa kujigonga kichwa kwenye ukuta wa seli.

Kauli hiyo ilitofautiana na uamuzi wa Inspekta Jenerali wa polisi Douglas Kanja ambaye aliwasimamisha maafisa waliokuwa kazini katika kituo cha polisi cha Central alipowekwa seli.

Kabla ya kukamatwa, alikuwa amerejea nyumbani na mkewe alikuwa akijiandaa kumpa chakula polisi hao walipofika.

“Tuliwaambia waingie ndani ya nyumba lakini walikataa wakisema walikuwa wakimtafuta Ojwang,” akasema Bw Opiyo.

Polisi hao waliambia familia hiyo alikuwa akisakwa kutokana na chapisho kwenye ukurasa wake wa X lililomhusisha afisa mmoja wa ngazi ya juu katika idara ya polisi kwa kushiriki ufisadi.

Bw Ojwang’ alikamatwa, akatiwa pingu na kusafirishwa kwa pikipiki hadi kituo cha polisi cha Mawego, Homa Bay. Kwa mujibu wa Bw Opiyo, familia yake ilimfuata lakini haikujua angesafirishwa hadi Nairobi na simu yake pia ilichukuliwa.

Polisi kituoni walimpa Bw Ojwang’ stakabadhi ya kurasa mbili ili atie saini, akafanya hivyo kisha akaandika jina lake na nambari ya kitambulisho.

Hata hivyo, familia yake haikuruhusiwa kusoma stakabadhi hiyo na hakukuwa na idhibati maelezo kumhusu yalikuwa yamenakiliwa kituoni humo.

Maafisa sita wa polisi walimweka Bw Ojwang’ kwenye gari nyeusi lenye nambari ya kibinafsi kisha wakaondoka na wakaihakikishia familia kuwa mwanao angekuwa salama.

Babake marehemu, Bw Meshack Opiyo jioni hiyo aliabiri gari la kuelekea Nairobi lakini hata kabla yake kufika familia ilipokea habari Bw Ojwang’ alikuwa amekufa.

Jana, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula aliamuru Kamati ya Bunge Kuhusu Usalama kuwasilisha ripoti kuhusu uchunguzi na asasi husika kuhusu chanzo cha kifo cha mwanablogu Albert Ojwang, Alhamisi alasiri.

“Kwa sababu hilo ni suala ambalo limevutia hisia kitaifa, Bw Gabriel Tongoyo naamuru kamati yako kutoa ripoti ya awali kuhusu uchunguzi unaoendeshwa na IPOA kuhusu kifo cha Ojwang Alhamisi saa nane na nusu alasiri. Ripoti hiyo itawasilishwa kabla ya Waziri wa Fedha kusoma makadirio ya bajeti,” Bw Wetang’ula akasema.

Kwa upande wake, Bw Tongoyo, ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Usalama na mbunge wa Narok Magharibi, alisema tayari kamati yake imewaagiza Inpekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na mwenyekiti wa Mamlaka ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) Isaack Hassan kufika mbele yake leo kuelezea kile ambacho wanafanya kubaini ukweli kuhusu kisa hicho.

“Tayari Karani wa Bunge amewaandikia barua Inspekta Jenerali na mwenyekiti wa IPOA kufika mbele ya kamati yetu kutoa ufafanuzi kuhusu kifo cha Ojwang’. Wabunge waliouliza maswali kuhusu suala hili wahudhurie vikao vya kamati yangu siku hiyo Jumatano, ili watusaidie katika kazi hii,” Bw Tongoyo akaeleza.

Awali, wabunge Eva Obara (Kabondo Kasipul), Esther Passari (Mbunge Mwakilishi wa Nairobi), Kagongo Bowen (Marakwet Magharariki na Jared Okello wa Nyando walishambulia polisi kuhusiana na kifo cha Ojwang’, ambaye pioa ni mwalimu.