Ombi wajukuu wa Moi wapimwe DNA kabla ya urithi
MVUTANO mpya wa kisheria umeibuka kuhusu urithi wa mali ya marehemu Jonathan Kipkemboi Moi, mwana wa aliyekuwa Rais Daniel arap Moi, huku baadhi ya wana wake wakitaka watoto wote 19 wanaodaiwa kuwa warithi wafanyiwe vipimo vya DNA ili kuthibitisha uhalali wao.
Wakiwa mbele ya Jaji wa Mahakama Kuu Eric Ogola, mke wa kwanza wa Jonathan, Sylvia Moi, pamoja na mwanawe Clint Kiprono Moi waliomba agizo la mahakama lililotolewa Agosti 2023, linalotambua watoto hao 19 kama warithi wa mali ya marehemu, liondolewe.
Sylvia na Clint waliambia mahakama kuwa ni lazima watoto wote waliotambuliwa kama warithi wapimwe DNA ili kuthibitisha kuwa wana damu ya ukoo wa marehemu Rais Moi.
Kwa mujibu wa Clint, Rais Moi aliweka wazi kwenye wosia wake kuwa ni wale tu wa damu yake wanapaswa kunufaika na urithi wa mali yake ya thamani ya mabilioni.
Katika wosia huo, uliothibitishwa na mahakama Jumanne, Moi alitoa asilimia 20 ya hisa za kila moja ya mali nne na akaunti mbili za benki kwa wanawe watano ambao ni marehemu Jonathan, Raymond, Gideon, Philip na John Mark.
Mwanawe akifariki, Moi alieleza kwamba sehemu ya urithi wa mwana huyo itachukuliwa na watoto wake wa damu.
“Ni muhimu sasa kuthibitisha warithi halali wa mali yote inayogawanywa katika urithi huu kwa sababu msimamizi wa urithi wa marehemu Rais Moi hataweza kugawa mali hiyo kwa warithi halali endapo hawatatambuliwa,” alisema Clint katika ombi lake.
Uamuzi wa maombi hayo unatarajiwa kutolewa na Jaji Ogola Juni 26, 2025.
Clint alisema hakuwepo wakati mpatanishi wa mahakama alipofanya uamuzi, ambapo walio wengi walishinda kwa kura, lakini baadhi ya watoto waliotajwa hawakuwa wanafahamika na familia.
Maombi hayo yalipingwa na baadhi ya warithi wa mali hiyo wakisema kuwa orodha ya warithi ilikubaliwa na pande zote kisha kupitishwa na Jaji Maureen Odera mnamo Agosti 4, 2023.
Mawakili Duncan Okatch na Pearlyne Omamo waliambia mahakama kuwa ombi hilo ni la kibaguzi kwani watoto wote 19 walitambuliwa kupitia mchakato wa upatanishi.
Bi Omamo alisema hakukuwa na ubishi kwamba watoto wanne kati yao hawakuwa wa damu ya Jonathan, lakini alikuwa akiwatunza kabla ya kufariki kwake.
Wakili huyo alieleza kuwa kuna mtoto mdogo ambaye ni mrithi na anahitaji matibabu ya haraka kwani anaugua saratani ya kiwango cha pili.
Bi Omamo alipendekeza kufunguliwa kwa akaunti ya pamoja ambapo fedha kutoka mali ya marehemu Moi zingeelekezwa ili kugharamia mahitaji ya dharura ya warithi.
Aliongeza kuwa warithi walikubaliana kwamba mali hiyo itumike kugharamia mahitaji ya dharura ya matibabu na ada za shule kwa warithi wote 19.
Katika hati ya kiapo, Bw Fredrick Kibichii ambaye pia ni mrithi, alisema ombi hilo halina msingi, ni la kibaguzi na linagawanya familia.
Bw Kibichii alisema makubaliano ya upatanishi wa awali yaliwekwa kama agizo la mahakama na mawakili wote wa familia zote nne, wakiwemo mawakili wa Sylvia na Clint.
Aliongeza kuwa kwa nia njema ya mchakato wa upatanishi, pande zote zilikubaliana kuachana na madai hayo na zoezi la kuwatambua warithi wa marehemu Jonathan lilikamilishwa kwa amani na familia zote nne kupitia makubaliano ya upatanishi wa sehemu.
“Hakukuwa na udanganyifu au kosa kama inavyodaiwa na walalamishi kuhusu watu 19 waliotajwa kuwa warithi. Hivyo walalamishi hawapaswi kufungua upya mambo yaliyokamilika kwa amani,” alisema Kibichii.
Aliongeza kuwa ombi hilo lilikuwa jaribio la kuzuia mchakato wa kugawa urithi na kuathiri warithi walio katika hali gumu, wakiwemo watoto wagonjwa wanaohitaji msaada wa kifedha wa haraka kwa matibabu na elimu.
Mpatanishi aliyeteuliwa na mahakama alifanya mikutano kadhaa na familia ya Jonathan kati ya Machi 31 na Aprili 18, 2023, na warithi 19 wakatambuliwa.
Kwa ajili ya haki, Jaji Odera aliamuru kila nyumba kati ya nne ipate mwakilishi miongoni mwa wasimamizi.
Familia ya Sylvia ilitakiwa kuchagua kati ya Clint au Sylvia kama mwakilishi, Beatrice Moi alimteua binti yake April Moi, Ashney Mary alichaguliwa kuwakilisha familia ya Faith, na Bw Fredrick Kibichii kuwakilisha familia ya nne.