Habari

Pigo kwa watafuta huduma vitambulisho 1,300 vilichomeka Nyandarua katika maandamano

Na ERIC MATARA June 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ZAIDI ya vitambulisho 1,300 ambavyo vilikuwa vikisubiri kuchukuliwa, viliharibiwa katika Kaunti ya Nyandarua baada ya kuchomwa kwenye maandamano ya Jumatano.

Waandamanaji waliokuwa na ghadhabu waliteketeza mali ya serikali ambayo thamani yake ni zaidi ya Sh40 milioni mjini Ol Kalou.

Katibu katika Wizara ya Uhamiaji Dkt Belio Kipsang, alifichua kuwa vitambulisho hivyo viliharibiwa baada ya waandamanaji kuteketeza moto afisi ya Usajili wa Takwimu ya Kitaifa kwenye kaunti ndogo ya Nyandarua ya Kati.

“Hii itavuruga shughuli katika eneo hilo kwa sababu wakazi wanategemea vitambulisho kupata huduma bora kama za afya, elimu, benki na ajira. Ni pigo sana kwa wanaosaka huduma za umma,” akasema Dkt Kipsang’.

Aliongeza kuwa vifaa vya kielektroniki vya kutambua wale ambao wanatuma ombi la kupata kitambulisho na vifaa vingine vya serikali vya thamani ya Sh1 milioni, viliharibiwa kwenye moto huo.

Aidha Dkt Kipsang’ alifichua kuwa vitambulisho 900 zaidi viliibwa kutoka kwa afisi ya usajili wa watu Nyandarua Magharibi jijini Oljoroorok baada ya afisi kuvunjwa.

Naibu Kamishina wa Kaunti ndogo ya Nyandarua Magharibi Josephine Kihara alisema wizi huo ulitokea mnamo Mei 29, 2025.

Dkt Kipsang’ alikuwa akiongea baada ya kuzuru Kaunti ya Nyandarua kukagua uharibifu uliotokea ambapo alitaka uchunguzi zaidi ufanyike iwapo vitambulisho 1,300 viliteketea ama viliibwa kabla ya jengo la afisi hiyo kuchomwa na waandamanaji.

“Naomba yeyote aliyetuma ombi la kupata kitambulisho Ol Kalou na Oljoroorok apige ripoti kwa polisi kwa sababu stakabadhi zao zinaweza kutumika kwa shughuli za uhalifu,” akaongeza Dkt Kipsang.

Alikashifu uvamizi kwenye asasi za serikali pamoja na maafisa wa usalama wakati wa maandamano, akisema serikali haitavumilia tabia kama hiyo.

Kuchomwa kwa afisi za serikali na makao makuu ya kaunti, kulitokea baada ya polisi kupiga risasi na kumuua mwaandamanaji.

Pia magari 26 ya serikali ya kaunti na ya kitaifa yaliteketezwa pamoja na pikipiki 19 za serikali ya kaunti.

Makachero kutoka Idara ya Upelelezi Nchini (DCI), wanafanya uchunguzi kuhusu uvamizi huo ili kuwanyaka wale ambao walihusika.