Habari

Polisi aliyempiga risasi mchuuzi wa barokoa Nairobi akamatwa- NPS

Na CHARLES WASONGA June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

AFISA wa polisi aliyenaswa kwenye kanda ya video akimpiga risasi na kumuua mchuuzi mmoja katikati mwa jijini Nairobi, Jumanne, Juni 17, 2025, amekamatwa.

Kulingana na taarifa iliyotolewa na msemaji wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) Muchiri Nyaga, afisa huyo alikamatwa kufuatia agizo la Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja.

Bw Nyaga alisema afisa huyo muuaji atafikishwa mahakamani na kufunguliwa mashtaka ya mauaji kwa kukusudia.

“Huduma ya Kitaifa ya Polisi imegadhabishwa na kisa ambapo afisa wa polisi alimpiga risasi raia asiye na silaha kwa kutumia bunduki ya kupambana na fujo katikati mwa jijini la Nairobi Jumanne. Kufuatia kisa hicho, Inspekta Jenerali wa Polisi ameamuru kukamatwa mara moja na kushtakiwa kwa afisa huyo. Afisa huyo amekamatwa,” akaeleza.

Bw Muchiri pia alisema NPS haina uhusiano wowote na magenge ya wahuni walioonekana wakiwashambulia waandamanani kwa mipini ya jembe katikati mwa jiji la Nairobi.

“Huduma ya Kitaifa ya Polisi inalaani makundi hayo haramu. Watu kama hao watakabiliwa kwa mujibu wa sheria,” akasema huku akiongeza kuwa uchunguzi umeanzisha kwa lengo la kuwatambua wanachama wa genge hilo na kuadhibiwa kwao kwa mujibu wa sheria.

Hata hivyo, wakati wa fujo hizo polisi walionekana kuwa na ukuruba na wahuni hao kwani waliwasindikiza wakikabiliana na waandamanaji.

Kuuawa kinyama kwa mchuuzi huyo ambaye alikuwa akiuza barakoa katika barabara ya Moi, karibu na jumba la Kibiashara la Imenti, kumelaaniwa na Wakenya wa matabaka mbalimbali wakiwemo wabunge.

Kwenye kikao cha alasiri, wabunge wakiongozwa na kiongozi wa wengine Kimani Ichung’wah walitaka maafisa wa polisi kukoma kutumia nguvu kupitia kiasi dhidi ya raia wasio na silaha.

“Kisa cha leo (Jumanne), jijini Nairobi ambapo afisa mmoja alimuua kwa kumpiga risasi mchuuzi asiye na silaha yoyote ni cha kisitisha zaidi. Kwa mara nyingi tunawahimiza maafisa wetu wa polisi waendeshe majukumu yao kwa uangalifu na kitaalum na wakome kuwashambulia raia kwa risasi kiholela,” akasema Bw Ichung’wah ambaye ni mbunge wa Kikuyu.

Wengine waliolaani ukatili huo wa polisi ni kiranja wa Wachache Millie Odhiambo, Makali Mulu (Kitui ya Kati) na Mbunge wa Kajiado Kaskazini Onesmus Ngogoyo.

Mchuuzi huyo, ambaye jina lake halikubainika mara moja, ameuawa na polisi siku wakati ambapo wanaharakati walikuwa wakiandamana kushinikiza kukamatwa kwa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi aliyejiondoa kazini kwa muda, Eliud Lagat, kuhusiana na mauaji ya mwanablogu Albert Ojwang’.