Habari

Polisi wachunguza kisa cha mwanamume kujitia kitanzi akiwa seli

Na GEORGE ODIWUOR June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

POLISI katika Kaunti ya Homa Bay wanachunguza tukio ambapo mvuvi mwenye umri wa miaka 36 aliripotiwa kujitia kitanzi kwenye kituo cha polisi cha Kipasi eneobunge la Mbita.

Mwanamume huyo, Calvins Omondi Onditi, alijitia kitanzi Jumapili asubuhi akitumia long’i yake baada ya kukamatwa usiku wa manane.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Homa Bay Lawrence Koilem, mwanamume huyo huenda aliamua kujitia kitanzi baada ya kulemewa na aibu. Onditi alikuwa mvuvi kwenye ufuo wa Ndhuru na alifumaniwa akiwa uchi kwenye zizi la mbuzi katika kijiji cha Ndhuru.

Baada ya kufumaniwa, wakazi wa eneo hilo walimwita chifu ambaye aliwaarifu polisi waliokuja na kumnyaka.

“Huenda aliabika kutokana na kile jamii yake ingesema akirejea nyumbani. Alifunga long’i vizuri na kuitumia kujitia kitanzi,” akasema Bw Koilem.

Familia yake ilikiri kuwa alifumaniwa na mbuzi lakini wakakanusha kuwa alijitia kitanzi huku wakisema alikuwa na tabia nzuri.

Marehemu ana mke na watoto na alipatikana kwenye zizi la mbuzi. Familia yake inatoka Kodiera, Ndhiwa lakini alihamia Ndhuru ambako amekuwa akiendeleza uvuvi.

Binamu yake Geoffrey Ochieng’ Ouma alikuwa kati ya watu ambao walienda eneo la tukio baada ya mwanaume huyo kufumaniwa na wakati huo alionekana kuwa mlevi.

“Alituambia aliwekwa kwenye zizi la mbuzi lakini nia yake haikuwa hapo. Mkulima hakulalamikia chochote kwa sababu hakupoteza chochote na alifahamu Omondi,” akasema Bw Ouma.

Mwili wa marehemu ulipelekwa hadi makafani ya Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Kaunti ya Homa Bay huku longí yake ikiwa bado shingoni baada ya kukatwa kutoka kwenye paa.