Habari

Polisi wafumania magunia 600 ya mbolea feki kwa Agrovet Eldoret

Na STEVE KETER February 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

POLISI jijini Eldoret Jumamosi walitwaa zaidi ya magunia 600 inayoshukiwa kuwa mbolea ghushi kwenye duka moja eneo la Naiberi barabara ya Eldoret-Kaptagat.

Maafisa hao waliendesha operesheni hiyo huku msimu wa upanzi nao ukinukia.

Naibu Kamishina wa Kaunti ya Uasin Gishu Patrick Wekesa alisema mbolea hiyo ilikuwa imepakiwa kwenye magunia ya kilo 60 na ilikuwa ya aina ya DAP.

Mbolea hiyo ilikuwa imenunuliwa kutoka kwenye bohari ya Bodi ya Kitaifa ya Nafaka na Mazao Eldoret kabla ya kuvurugwa.

“Uchunguzi wa awali unaonyesha mbolea ilinunuliwa kutoka kwa NCPB kisha ikawekwa kemikali isiyojulikana na ikapakiwa tena kwenye magunia ya DAP,” akasema Bw Wekesa.

“Huu ni uhalifu wa kiwango cha juu kiuchumi na si hadaa tu kwa wakulima bali pia inatishia usalama wa chakula eneo hili,” akaongeza Bw Wekesa.

Kwa mujibu wa polisi, mshukiwa kwenye sakata hiyo amekuwa akinunua mbolea kwa Sh2,500 kwa kila gunia kutoka NCPB kisha anaipakia upya kwenye magunia na kuuza kwa Sh6,000 kwa kila gunia.

Mwenye duka hilo Kotut Balers anayehusishwa na sakata hiyo bado hajakamatwa na anaendelea kusakwa na maafisa wa usalama.

Kutwaliwa kwa mbolea hiyo kunatokea wakati wakulima nao wanajiandaa kwa msimu wa upanzi na kuibua wasiwasi huenda wakulima wakauziwa mbolea ghushi.

Seneta wa Uasin Gishu Jackson Mandago naye amewataka wakulima wawe makini ili wasiuziwe mbolea feki.

“Wamakinike wanaponunua mbolea kwa sababu ile feki inayouzwa itachangia wao kuyapata mazao duni,” akasema Bw Mandago.

Polisi pia wamewaonya wale ambao walinunua mbolea kwenye duka hilo wazithibitishe na NCPB kufahamu iwapo ni halali.