Polisi washindwa kushawishi korti kuzuilia mwanamume anayedaiwa kutishia Seneta Hezena
MFANYABIASHARA amefikishwa kortini kwa madai ya kutishia kumuua Seneta Maalum wa Samburu Hezena Lemaletian.
Alex Anyolo Kikuyu aliyefikishwa mbele ya hakimu mkuu mahakama ya Milimani Lucas Onyina alikana madai ya Polisi kwamba “hana makazi Nairobi anaishi ndani ya gari lake.”
Bw Kikuyu aliambia mahakama kwamba ameoa na wamejaliwa kuwa na watoto wawili.
“Naomba kueleza hii mahakama kwamba mimi naishi mtaa wa Buruburu Nairobi. Siishi ndani ya gari,” alisema Bw Kikuyu huku akiomba mahakama imwachilie kwa dhamana.
Akiomba korti iamuru Bw Kikuyu azuiliwe kwa siku tano katika kituo cha polisi cha Muthaiga, Kachero George Ndung’u alisema alipomtia nguvuni alimpata akiwa na kadi za simu za Safaricom 23 na kadi nyinge za Airtel kumi (10).
Pia Bw Kikuyu na simu tatu za kiunga mbali na gari nambari ya usajili KBJ 795 Q.
Mahakama ilielezwa polisi wanahitaji kukamilisha uchunguzi.
Lakini Bw Kikuyu alipinga ombi hilo la kuzuiliwa siku tano, akisema gari lake na simu zake na kadi 43 za simu zote zimetwaliwa na polisi.
Alieleza mahakama kwamba polisi wamemfedhehesha wakidai anaishi ndani ya gari “jinsi ndege inavyoishi ndani ya kiota.”
Aliongeza kusema “mimi nimeoa na ninaishi Buruburu.”
Aliomba aachiliwe kwa dhamana akisema “siku tano ni nyingi. Nikisukumwa jela siku tano familia yangu itaumia. Inanitegemea mimi. Nilitiwa nguvuni Ijumaa wiki iliyopita niachilie kwa dhamana.”
Akitoa uamuzi, Bw Onyina alisema kulingana na jinsi mshtakiwa anavyoonekana “yeye ni mtu mwenye heshima zake na hawezi kuwa anaishi ndani ya gari.”
Aliamuru polisi wakamilishe ushahidi wao bila kuingilia maisha ya mshukiwa huyo.
Alimwachilia kwa dhamana ya Sh20,000.