Habari

Polisi wawili wafariki baada ya gari lao kugongana ana kwa ana na lori

Na SHABAN MAKOKHA June 3rd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MAAFISA wawili walikufa papo hapo katika ajali iliyohusisha gari lao la kazini na lori katika barabara ya Eldoret-Malaba eneo la Matulo, Bungoma.

Maafisa hao wawili kutoka kituo cha Railways, Bungoma walikuwa wakielekea upande wa Bungoma pale gari lao lilipogongana ana kwa ana na lori lililokuwa likiendeshwa kwa kasi likielekea Webuye, kutoka mpaka wa Malaba.

Kamanda wa Kaunti Ndogo ya Bungoma Kusini Rodgers Bosire alithibitisha kisa hicho kilichomwacha dereva wa lori hilo na majeraha mabaya na kukimbizwa hospitalini.

Wakazi walioshuhudia kisa hicho wanasema kwamba magari hayo mawili yalikuwa yakiendeshwa kwa kasi sana yalipogongana.

“Gari la polisi lilikuwa linajaribu kupita gari jingine wakati lilipogongana ana kwa ana na lori,” akasema Bw Julius Wekesa, mkazi.

Wakazi pia walilaumu serikali kwa kukosa kujenga matuta ya kusaidia magari kupunguza kasi kwenye eneo hilo ambalo sasa linaibuka kuwa hatari.

“Tunashuhudia ajali nyingi sana katika eneo hili. Wiki haipiti bila ajali. Serikali inafaa kujenga matuta ya barabarani,” akasema Bw Wekesa.