Habari

Presha kwa Mbadi akijiandaa kusoma bajeti

Na JUSTUS WANGA May 31st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Fedha John Mbadi anakabiliwa na changamoto ya kipekee anapojiandaa kuwasilisha bajeti yake ya kwanza tangu kuteuliwa kwake wakati uchumi wa nchi ungali unazongwa na mzigo mzito wa madeni.

Baada ya majuma mawili, Mbunge huyo wa zamani wa Suba Kusini atawasili bunge bajeti ambayo itaamua mkondo wa kiuchumi wa wa taifa hili.

Aidha, bajeti hiyo itaamua hatima yake kisiasa, kumjenga katika serikali ya Rais William au kumbomoa.

Kazi yake inakabiliwa na changamoto za kisiasa presha za kichumi na sifa mbaya ya utendakazi wa mtangulizi wake Njuguna Ndung’u.

Kwa mfano, Mswada wa Fedha wa 2025, uliotayarishwa na Profesa Njuguna ulichangia kupika kwa maandamano makubwa kote nchini.

Chama cha Mawakili Nchini (LSK) na Taasis ya Wahasibu Nchini (ICPAK) zimehimiza kwamba utayarisha wa bajeti ufanywe kwa njia ya uwazi na inayoziba mianya ya ubadhirifu na kuendeleza matumizi mazuri ya fedha za ushuru.

Bw Mbadi ambaye ni mwenyekiti wa zamani wa chama cha ODM anatarajiwa kusoma bajeti ya zaidi ya Sh4 trilioni mnamo Juni 12, 2025.

Nchi ya Kenya nayo inazongwa na mzigo wa madeni wa kima cha Sh11.02 trilioni ambayo kulipwa kwake kunategemea hakuchangii maendeleo ya kitaifa.

Bw Mbadi anakubali kuwa anawekewa presha Wakenya wakitaka kuona matunda ya utendakazi wake.

“Ndio kuna presha lakini haiwezi kutuzuia kufanya kazi,” Bw Mbadi akaungama.

“Unapokubali kuchukua uteuzi kushikilia nyadhifa kama hii kubwa, sharti uwe tayari kupata presha. Niko tayari kupambana na changamoto hizo kando na kumulikwa zaidi na umma,” akaambia Taifa Leo.

Bw Mbadi wananchi wanafaa kujua kuwa shughuli ya kutengenezwa kwa bajeti haifanywi na mtu mmoja. Badala yake inahusisha serikali yote na “hii ndio maana shughuli hii ilianza mwaka jana.

Waziri alisema haiwezekani kwa pesa kutoka hazina ya kitaifa kutimizwa matakwa ya kila Mkenya.

“Hauwezi kupata kila kitu unachotaka na kurejesha uchumi katika hali yake ya zamani. Kwa njia hiyo, presha nyingi zinazonizonga wakati huu zitapata suluhu. Baadhi ya matakwa hayo ni mazuri, ni muhimu lakini hatuwezi kumudu kuyafadhili sasa,” akaeleza kwenye mahojiano katika afisi yake.

Bw Mbadi aliongeza hivi: “Sharti nijulishe taifa kwamba hatufanyi kazi pekee yetu. Mambo ni magumu katika kiwango ulimwengu, sharti tutafute pesa za kuendesha uchumi bila kuongeza viwango vya ushuru.”

Juzi waziri alisema huenda Kenya ikikosa pesa za maendeleo ikizingatiwa kuwa Mamlaka ya Kitaifa ya Mapato (KRA) inakusanya Sh2.5 trilioni ilhali serikali inatumia Sh1.1 trilioni kulipia mikopo.

“Kwa hivyo, tutapata wapi pesa za kufadhili miradi ya maendeleo?,” Bw Mbadi akasema juzi, akiongeza kuwa mishahara pekee ya wafanyakazi wa umma hufyonza Sh960 bilioni kila mwaka.

Mswada wa Fedha wa 2024 ambao serikali ilitarajia kuutumia kupata jumla ya Sh347 bilioni, ilizimwa kufuatia maandamano ya vijana wa Gen Z ambayo kilele chake kilikuwa kuvamiwa kwa majengo ya bunge la kitaifa mnamo Juni 25, 2024.