Habari

Raila: Msamaha wa Ruto uandamane na fidia kwa wahanga wa ghasia za Juni 25

Na CECIL ODONGO June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa ODM Raila Odinga Jumapili alisema kuwa msamaha ambao Rais William Ruto aliomba wiki jana unastahili kuandamana na vitendo, akiitaka serikali ilipe fidia kwa familia za Gen Z ambao waliuawa au kujeruhiwa wakati wa maandamano ya mwaka jana.

Akiongea wakati wa maadhimisho ya 62 ya Madaraka, Bw Odinga pia alisema waliojeruhiwa au kuuawa wakati wa maandamano baada ya uchaguzi mkuu wa 2022 pia wanastahili kulipwa fidia.

Rais Ruto mnamo Jumatano wakati wa ibada ya kila mwaka ya kuombea nchi aliwaomba Gen Z msamaha na kutoa wito kwao waungane naye katika kujenga nchi.

“Miaka miwili iliyopita tulikuwa barabarani na mwaka jana Gen Z walikuwa barabarani. Mapema wiki hii wewe na Spika (Moses Wetangúla) mliomba msamaha kwa Gen Z na hilo ni muhimu,

“Kuna wale walikufa na waliojeruhiwa. Ningependa kusema familia zao zilipwe fidia ili suala hili liishe kwenye historia ya taifa letu na Wakenya waishi kwa amani na umoja,” akasema Bw Odinga.

Aidha kiongozi huyo alisema Homa Bay ni mfano tosha kuwa ugatuzi umefaulu kutokana na miradi mbalimbali ambayo imetekelezwa eneo hilo na kaunti.

“Hii siku imeonyesha kuwa ugatuzi unafanya kazi na unaweza kufanya kazi zaidi iwapo utaungwa mkono na serikali ya juu,” akaongeza Bw Odinga.

“Serikali inafaa kuzipa kaunti rasilimali tosha na huduma ambazo bado hazijagatuliwa bado zinaweza kufikishwa kwa raia. Rais nakuomba usifufue utawala wa mkoa na tungependa magavana wapate rasilimali tosha za kufanya kazi yao,” akasema waziri huyo mkuu wa zamani.

Aliendelea kuwapiga debe magavana kusimamia hazina mbalimbali ikiwemo ile ya Hazina ya Kifedha ya Ustawi ya Maeneobunge Nchini (CDF).

Kumekuwa na mgawanyiko mkubwa kuhusu suala hilo wabunge wakiapa kuwa hawatawaachia magavana hazina hiyo iendeshe.

Pia Bw Odinga amekuwa akipigania magavana wapewe pesa za kujenga barabara mashinani ambazo zimekuwa zikisimamiwa na barabara kuu.

Kama kawaida yake, Bw Odinga alirejelea historia ya ukombozi wa nchi huku akisema Kenya lazima iishi ndoto ya waanzilishi wa taifa hili.

Bw Odinga akimalizia aliwaambia wafuasi wake waendelee kuwa nyuma yake huku akisema anafahamu mahali waliko sasa na mwelekeo ambao watauchukua kisiasa kuelekea kura ya 2022.