Habari

Raila ataka serikali iwajibike kuhusu kifo tata cha mwalimu-bloga Albert Ojwang’

Na WINNIE ONYANDO June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KIONGOZI wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Raila Odinga amelaani kifo cha mwalimu Albert Ojwang’ ambaye kifo chake kimezua taharuki nchini.

Bw Odinga sasa anaitaka serikali ya Rais William Ruto kuwajibika ili haki itendeke kwa familia ya mwathiriwa.

Haya yanajiri huku uchunguzi ukiendelea kuhusu kifo tata cha mwanamitandao huyo.

Upasuaji wa maiti uliofanywa Jumanne Juni 10, 2025 unaonyesha kuwa kijana huyo alikuwa na majeraha kichwani, shingoni na sehemu zingine za mwili wake.

Bw Ojwang’ alikamatwa kwao nyumbani mnamo Jumanne, na watu sita ambao walijitambulisha kama maafisa wa polisi wakiwa kwenye pikipiki tatu.

“Wawili waliingia kupitia ua wa nyuma kisha wa tatu akatumia lango la mbele. Wengine walizingira boma kana kwamba hawakuwa wakitaka mtu atoroke,” akasema Herman Ojwang’ mjomba wa marehemu.

Polisi hao waliambia familia hiyo alikuwa akisakwa kutokana na chapisho kwenye ukurasa wake wa X lililomtuhumu afisa mmoja wa ngazi ya juu kwenye idara ya polisi kwa kushiriki ufisadi.

Bw Ojwang’ alikamatwa, akatiwa pingu na kusafirishwa kwa pikipiki hadi kituo cha polisi cha Mawego.

Kwa mujibu wa Bw Opiyo, familia yake ilimfuata lakini haikujua angesafirishwa hadi Nairobi na simu yake pia ilichukuliwa.

Kifo chache uliotokea muda mfupi baada ya kufikishwa Nairobi umezua wasiwasi nchini huku viongozi mbalimbali wakiitaka serikali kuwajibika.