Ruth Odinga akutana na kakake Oburu mzozo ODM ukiendelea
MBUNGE mwakilishi wa jinsia ya kike Kaunti ya Kisumu Ruth Odinga amemtembelea kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) Oburu Odinga huku kukiwa na madai ya migawanyiko ndani ya chama hicho.
Kupitia taarifa aliyochapisha kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii Alhamisi, Machi 5, 2026, Ruth ambaye pia ni Katibu wa Uratibu wa ODM, alisema mazungumzo yao yalilenga kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya chama pamoja na mikakati ya kupeleka mbele ajenda za kitaifa.
“Leo alasiri nilifanya ziara ya heshima katika afisi ya kiongozi wa chama cha ODM, Oburu Odinga, nikiwa na Mheshimiwa Catherine Omanyo. Tulikuwa na mazungumzo ya maana kuhusu kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya chama na kuendeleza malengo ya kitaifa yanayowahusu Wakenya wote,” alisema.
Ruth alikuwa ameandamana na Omanyo ambaye ni naibu katibu mkuu wa chama hicho. Omanyo alipandishwa cheo hivi majuzi baada ya kuondolewa kwa Edwin Sifuna, hatua ambayo baadaye ilibatilishwa na Jopo la Kutatua mizozo ya vyama vya kisiasa (PPDT).
Ziara hiyo ilijiri huku kukiwa na madai kwamba kuna mvutano kati ya Ruth na kaka yake, Oburu. Hata hivyo, alikanusha madai hayo akisema wito wake wa kutaka utaratibu ndani ya ODM haufai kuchukuliwa kama ugomvi kati yake na kaka yake.
Alisema hana sababu ya kupigana na kiongozi huyo wa chama, akieleza kuwa wito wake umekuwa kuhimiza makundi ya “Wantam” na “Tutam” ndani ya chama kushirikiana na kuzungumza kwa sauti moja.
Ruth pia alisisitiza kuwa sauti za vijana zinapaswa kujumuishwa katika maamuzi ya chama, akisema hilo halipaswi kuchukuliwa kama dharau kwa seneta huyo wa Siaya.
Alifafanua kuwa mara nyingi humshauri Oburu kuhusu masuala mbalimbali ya chama na kisiasa, akiongeza kuwa kutoa maoni yake ndani ya chama cha kidemokrasia kama ODM hakumaanishi kuwa anapinga uongozi wake.
“Oburu ndiye kiongozi wa chama cha ODM na kila mtu anapaswa kuheshimu hilo. Ninazungumza naye mara kwa mara kama kiongozi wa chama na pia kama kaka yangu mkubwa. Lakini baadhi ya watu wameeneza wazo kwamba ninapigana naye,” alisema.
Aliongeza kuwa wanaodai anagombana na Oburu ndio maadui wa kweli wa ODM kwani chama hicho kinaruhusu wanachama wake kutoa maoni yao kwa uhuru.