Ruto kuelekea Uingereza na Uhispania kutia saini mikataba ya kuiletea Kenya vinono
RAIS William Ruto anaondoka nchini Jumapili, Juni 29, 2025 kwa ziara rasmi katika mataifa ya Uingereza na Uhispania anakotarajiwa kutia mikataba kadhaa ya ushirikiano wa kimaendeleo kati ya Kenya na nchi hizo za Uropa.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed majira ya asubuhi, Dkt Ruto akiwa Uingereza, atatia saini Mkataba mpya wa Ushirikiano wa Kimkakati kati ya Kenya na Uingereza utakaodumu kati ya 2025 hadi 2030.
“Mkataba huo unatarajiwa kufungua milango ya uwekezaji nchini Kenya, nafasi za ajira na kuifanya Kenya kuwa eneo bora ulimwenguni kibiashara, kiteknolojia na kiusalama,” akaeleza.
“Rais Ruto ataungana na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer jijini London kutia saini mkataba huo wa ushirikiano uliohimiliwa katika nguzo nne za; biashara, hali ya anga, teknoloji na usalama,” Bw Mohamed akaeleza.
Ushirikiano huo, akasema, unalenga kuimarisha, maradufu, biashara kati ya Kenya na Uingereza, kuwezesha Wakenya zaidi kupata ujuzi wa kidijitali na kuimarisha ushirikiano kuhusiana na usalama wa kikanda kwa kukabiliana na ugaidi, uhalifu wa mtandaoni na athari za mabadiliko ya tabia nchi.
“Chini ya nguzo ya biashara na ustawi wa miradi isiyochafua mazingira, Kenya na Uingereza itatoa kipaumbele kwa ukamilishaji wa miradi kama ule wa uchukuzi wa reli jijini Nairobi. Uingereza pia inalenga kutoa hadi pauni 1.5 bilioni (Sh266 bilioni) kufadhili miradi mbalimbali nchini kufikia 2030,” Bw Mohamed akaongeza.
Kabla ya kuwasili London, Dkt Ruto atatua jijini Seville, Uhispania ambako atahudhuria kongamano la kimataifa kuhusu ufadhili wa maendeleo.
Kongamano hilo la Nne kuhusu Ufadhili wa Maendeleo utawaleta pamoja viongozi wa kutoka mataifa mbalimbali ulimwenguni kujadili misingi mipya ya ufadhili wa miradi ya maendeleo.
“Rais anatarajiwa kutumia jukwaa hilo kutoa wito kwa ushirikiano wa mataifa ya ulimwengu katika kushughulikia changamoto kuu kama vile umasikini, kudorora kwa chumi za nchi mbalimbali, mabadiliko ya tabia nchi na kuangamia kwa viumbe asili, miongoni mwa mengine,” akasema Bw Mohamed.