Habari

Sababu zilizopelekea Ruto kufuta ziara yake ya Migori kabla ya Madaraka Dei

Na MOSES NYAMORI May 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MVUTANO wa mamlaka kati ya Gavana wa Migori Ochilo Ayacko na viongozi wengine waliochaguliwa umemlazimu Rais William Ruto kufuta ziara yake katika kaunti hiyo.

Kiongozi wa Taifa aliratibiwa kuzuru Migori Alhamisi, Mei 29 kabla ya kuelekea Homa Bay na Kisumu Ijumaa na Jumamosi mtawalia, kuzindua miradi ya maendeleo kabla ya sherehe za kuadhimisha Sikukuu ya Madaraka.

Bw Ayacko jana alijipata mpweke kufuatia madai kuwa alijaribu kuwatenga viongozi wengine waliochaguliwa kwenye ziara ya Rais.

Imeibuka kuwa Dkt Ruto alipozuru Migori mapema mwezi huu, madiwani walimwomba kuwakaribisha ikulu kwa kikao cha majadiliano.

Kisha gavana akamwomba Rais kuwakaribisha viongozi wote waliochaguliwa kutoka eneo hilo, ombi ambalo Dkt Ruto alikubali.

Hata hivyo, Gavana anashutumiwa kwa kukataa kushirikisha viongozi wengine katika maandalizi ya ziara hiyo.

Ubaguzi huo unaodaiwa ulisababisha sehemu kubwa ya wabunge kutoka eneo hilo kushiriki kikao Jumanne Nairobi ambapo waliafikiana kususia ziara ya rais kulalamika.

Kikao hicho kiliongozwa na Kiongozi wa Wachache Bungeni, Junet Mohammed na kuhudhuriwa na wabunge wote isipokuwa Mwakilishi Mwanamke Mohammed Fatuma na mbunge wa Suna Magharibi Peter Masara.

Matukio hayo yalimlazimu Kiongozi wa Nchi kubadilisha ratiba yake na kufuta Migori.

Ikulu kupitia Mkuu wa Mawasiliano ya Rais, Munyori Buku, alithibitisha manadiliko hayo kwenye mipango ya rais.

Bw Mohammed alithibitisha vilevile mabadiliko kwenye ratiba lakini hakueleza kwa kina.

“Ziara imeahirishwa kwa sababu ya shughuli zitakazofanyika Kisumu siku hiyo hiyo,” alisema Bw Mohammed.