Habari

Samidoh anayesakwa kwa kuhepa kazi yake ya polisi kuendelea kupiga Mugithi Amerika

Na NYABOGA KIAGE June 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWANAMUZIKI maarufu wa Mugithi, Samuel Muchori almaarufu Samidoh, huenda asiripoti kazini Gilgil hivi karibuni licha ya agizo rasmi la polisi.

Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) imemlaumu Samidoh kwa kutelekeza kazi katika Kitengo cha Kukabiliana na Wizi wa Mifugo (ASTU), ambako alihamishiwa na wakuu wa polisi waliokerwa na moja ya maonyesho yake ambapo mashabiki walikuwa wakiimba kauli ya kisiasa “Wantam”.

Kwa mujibu wa taarifa ya ndani ya polisi iliyotiwa saini na Kennedy Barasa kwa niaba ya mkuu wa ASTU, Joseph Limo, Samidoh alitakiwa kuripoti kazini Mei 27, lakini hadi sasa hajafanya hivyo.

Mnamo Jumanne usiku, Samidoh alichapisha ratiba ya maonyesho yake ya muziki nchini Amerika mwezi Juni na Julai.

Katika chapisho lenye ujumbe wa mafumbo lililowekwa baada ya amri hiyo ya polisi, Samidoh aliorodhesha maeneo atakayotumbuiza – Houston, Texas, Massachusetts, Dallas na Washington.

Alimalizia na methali kwamba “hata tai huruka juu angani, huteremka kutafuta chakula. Methali ya wenye hekima.”

Polisi wanasema alipewa ruhusa ya mapumziko lakini hajarudi kazini kama ilivyokubaliwa.

“Afisa alipewa likizo lakini alitakiwa kurudi kazini Mei 27 2025. Tangu wakati huo hajaonekana na juhudi za kumtafuta hazijazaa matunda,” inasema taarifa hiyo ya ndani ya polisi.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa kutofika kwake kazini kwa zaidi ya siku 10 kulipelekea kutangazwa kuwa ameacha kazi (deserter), na mshahara wake ulisitishwa mara moja.

Polisi wa Gatumbiro, Kaunti ya Nyandarua, pia waliagizwa kutembelea nyumbani kwake na kupata taarifa kuhusu alipo.

Hata hivyo, barua nyingine kutoka NPS iliyoibuka baadaye ilionyesha kuwa Aprili 25, Samidoh alipewa ruhusa ya kusafiri kwenda Amerika kuanzia Mei 20 hadi Juni 9.

Taifa Leo ilijaribu kuwasiliana na Samidoh, lakini hakujibu maswali yetu.

Kwa mujibu wa Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi kuacha kazi ni kosa la jinai.

“Afisa wa polisi akikosa kufika kazini bila ruhusa au sababu halali kwa kipindi kinachozidi siku kumi, atachukuliwa kuwa ametoroka kazi isipokuwa athibitishe vinginevyo.”

Kifungu cha 94(3) kinaongeza kuwa: “Afisa yeyote wa polisi anayetoroka kazi atakuwa ametenda kosa na anaweza kufukuzwa kazi au kuhukumiwa kifungo kisichozidi miaka miwili.”

Kabla ya kuelekea Amerika, Samidoh alifanya maonyesho Uingereza na Ireland.

Mnamo Mei 28, alikuwa Southall, London, na aliandika kwenye mitandao ya kijamii akisema: “Mti haulaumu shoka; hukua juu ya jeraha na kuendelea kukua zaidi.”

Siku iliyofuata, alichapisha nukuu ya mapinduzi kutoka kwa Thomas Jefferson: “Haki inapotawaliwa na sheria ya dhuluma, basi upinzani huwa ni wajibu.”

Kuhamishwa kwake ASTU kulizua mjadala mitandaoni, lakini Inspekta Jenerali Douglas Kanja alieleza kuwa maafisa wote wa umma huhamishwa mara kwa mara, na Samidoh hakuwa tofauti.