Habari

Sekta ya majanichai yaonyesha ukuaji huku ikiandikisha Sh218.79b sokoni katika bajeti ya mwaka jana

Na NA VITALIS KIMUTAI April 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SEKTA ya majanichai nchini imeonyesha ukuaji kwa kiasi kikubwa, ikiandikisha thamani ya Sh218.79 bilioni sokoni katika bajeti ya mwaka uliopita.

Ukuaji huo umehusishwa na mikakati thabiti ya mauzo na mageuzi yanayoungwa mkono na serikali ambayo yamepanua soko la Kenya kimataifa kutoka masoko 96 hadi 100 ya kuuza mazao hayo ng’ambo.

Kulingana na ripoti ya Utendakazi wa Sekta ya majanichai iliyotolewa na Bodi ya Majanichai Nchini (TBK), Alhamisi, mapato ya sekta hiyo yaliongezeka hadi kufikia Sh186.91 bilioni 2025, kutoka Sh181.69 bilioni 2024, nyongeza ya asilimia 2.87 inayowakilisha Sh5.22 bilioni kwenye mapato ya ziada.

Kiasi cha mazao yaliyouzwa Ulaya kilipanda vilevile kutoka kilogramu 652.80 milioni, nyongeza ya asilimia 9.81 kutoka kilogramu 594.50 milioni 2024, kiasi kilichopanda kwa kilogramu 58.3 milioni.

Mauzo ya humu nchini yalipanda kwa asilimia sita kufikia Sh19.13 bilioni huku thamani ya mauzo ya majani chai kwa jumla ikiongezeka kwa asilimia mbili kutoka Sh215.21 bilioni 2024 hadi Sh218.79 bilioni 2025.

Wakulima 700,000 wanaomiliki mashamba madogo madogo walichangia kilogramu 272.77 milioni, kampuni za majanichai zilizalisha kilogramu 135.5 milioni, mashirika huru kilogramu 138.818 milioni huku Maeneo ya Majani Chai ya Nyayo yanayomilikiwa na serikali yakichangia kilogramu 4.24 milioni.

Matokeo haya ni afueni kuu kwa wadau baada ya matokeo duni ya 2023 na 2024 yaliyosababisha tani zaidi ya 100 milioni kukosa soko kwenye Mnada wa Majanichai Mombasa, na kufanya bei kudorora.

Waziri wa Kilimo, Mutahi Kagwe alisema sekta hiyo inaimarika na kuwahimiza wakulima kuzingatia mbinu bora za kilimo ikiwemo uchumaji bora wa majani mawili na kijani chipukizi, ili kustawisha ukuaji wa mapato ya kigeni.

Alisema haya katika kiwanda cha majani cha Rukuriri, Embu, akitoa ripoti hiyo.

“Matokeo haya siyo ya kubahatisha ila ni matokeo ya mageuzi ya kimaksudi, upanuzi wa soko na uzingatiaji upya kuhusu kuimarisha ubora na thamani chini ya ajenda ya Mabadiliko Kiuchumi kuanzia Mashinani,” alisema Waziri Kagwe.

Haya yanajiri huku kero la mapinduzi ya mara kwa mara linalogubika uongozi wa bodi ya Halmashauri ya Majani Chai Nchini (KTDA) likijitokeza tena kufuatia kufurushwa kwa mwenyekiti Chege Kirundi.

Mwenyekiti hushikilia afisi kwa miaka mitatu, lakini katika kipindi cha miaka minne iliyopita, bodi hiyo imefanyiwa mageuzi mara nne – idadi kubwa zaidi katika siku za hivi majuzi.

Katika mabadiliko mapya, mwenyekiti wa bodi wa zamani, Enos Njeru amerejea katika kile kinachoashiria misukosuko ya uongozi kwenye bodi iliyotwikwa jukumu la kuongoza masuala ya wakulima 700,000 wa majani chai.

Mabadiliko hayo yalitangazwa na KTDA Machi 4 huku athari za hatua hiyo zikichipuka.