Habari

Seneti yazua maswali kuhusu mkataba kati ya Ruto na Sakaja

Na MARY WANGARI March 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HATIMA ya mkataba wa ushirikiano wenye thamani ya Sh80 bilioni kati ya serikali kuu na serikali ya kaunti ya Nairobi ingali imegubikwa na suitafahamu huku Seneti ikidadisi masuala tata kadhaa, mwezi mmoja tangu muafaka huo utiwe saini rasmi.

Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi alikabiliwa na wakati mgumu Jumatatu kufafanua mchakato wa kufadhili kifedha mkataba huo na deni la Sh16 bilioni lililoachiwa serikali ya kaunti hiyo chini ya mpango wa awali wa Halmashauri ya Huduma Nairobi (NMS).

Aidha, kamati ya Seneti kuhusu Ugatuzi na Mahusiano baina ya Serikali iliitisha majibu kuhusu mchakato wa utekelezaji, majukumu mahsusi ya pande husika, ikionya kwamba muafaka huo unasheheni maelezo finyu.

Kamati hiyo inayoongozwa na Seneta Mohammed Abbas (Wajir) ilisema kuwa kipengee kuhusu fedha katika muafaka huo “ni chapwa.”

“Bado haujui Sh80 bilioni ziko wapi. Kipengee kuhusu fedha kinasema pande husika zitaafikiana kuhusu namna ya ufadhili. Kipengee hicho ni chapwa mno,” alisema Naibu Mwenyekiti wa Kamati, Catherine Mumma.