Habari

Serikali kuajiri walimu 40,000- katibu

Na MERCY SIMIYU NA LYNET IGADWAH June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

Serikali imetangaza mpango wa kuajiri walimu 40,000 ifikapo mwisho wa mwaka 2026 ili kuimarisha uwiano kati ya walimu na wanafunzi katika shule za umma.

Katibu wa Elimu ya Msingi, Julius Bitok, amesema walimu 24,000 wataajiriwa mwaka huu na walimu wengine 16,000 kuanzia mwaka ujao. Hii ni sehemu ya ahadi ya serikali kuajiri walimu 116,000 katika kipindi cha miaka mitano.

Kamati ya Bunge kuhusu Elimu imeshauri Sh1.3 bilioni zitolewe katika bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 ili kubadilisha walimu wanagenzi 20,000 kuwa wa kudumu kuanzia Julai.

Awali, Tume ya Huduma ya Walimu (TSC) ilieleza kuwa haikuwa imetengewa fedha za kuajiri walimu hao baada ya muda wao kumalizika.

TSC imesema kuna upungufu mkubwa wa walimu 98,261 nchini, hali inayotarajiwa kuwa mbaya zaidi ifikapo 2026 wakati shule za sekondari pevu zitakapoanzishwa. Aidha, kuna walimu 343,485 waliosajiliwa lakini bado hawajaajiriwa, wakiwemo walimu wa shule za msingi, sekondari na wale wa chekechea.

Waziri wa Elimu Julius Ogamba ameeleza kuwa uajiri wa walimu unategemea bajeti, upatikanaji wa fedha na nafasi zilizopo. Alisisitiza kuwa mpango wa mafunzo kwa walimu wasio na ajira umeimarisha ujuzi wa vitendo kwa walimu 94,300.

Katika miaka ya fedha 2022/2023 hadi 2024/2025, walimu 68,313 waliajiriwa kufundisha katika shule za msingi, wakiwemo wa kudumu na wa kandarasi. Hata hivyo, idadi ya walimu katika shule za msingi za umma ilipungua kwa asilimia 3.2 mwaka 2024, licha ya ongezeko la wanafunzi katika shule zote.

Akizungumza kwenye maadhimisho ya miaka 60 ya Shule ya Baringo, Katibu wa Elimu ya Msingi, Julius Bitok, alitangaza kuwa serikali itaajiri 24,000 walimu mwaka huu na 16,000 zaidi mwaka ujao, ili kutimiza ahadi ya kuajiri walimu 116,000 ndani ya miaka mitano chini ya mpango wa Kenya Kwanza.

Mwaka jana, walimu wa shule ya msingi walioajiriwa kwa kandarasi 39,550 walibadilishwa kuwa wa kudumu, na wengine 8,378 walihamishiwa kufundisha shule za sekondari msingi.

Kulingana na Ripoti ya Uchumi ya 2025, usajili wa wanafunzi umeongezeka katika viwango mbalimbali vya elimu:

Wanafunzi wa chekechea waliongezeka hadi milioni 2.914 mwaka 2024 kutoka milioni 2.885 mwaka 2023. Shule za msingi na sekondari msingi idadi ya wanafunzi iliongezeka kwa asilimia 3.2 hadi kufikia wanafunzi 10,733,300 mwaka 2024. Katika shule za sekondari idadi ya wanafunzi iliongezeka kwa asilimia 5.2 hadi wanafunzi 4,321,600 mwaka huo huo. Hata hivyo, idadi ya walimu katika shule za msingi za umma ilipungua kwa asilimia 3.2 hadi 212,602 mwaka 2024. Kwa upande mwingine, walimu katika shule za sekondari za umma na vyuo vya walimu waliongezeka kutoka 125,563 mwaka 2023 hadi 130,818 mwaka 2024.