Serikali kusaidia familia za Kiislamu msimu wa Ramadhan
SERIKALI ya kitaifa imeweka mpango wa kusaidia familia za Kiislamu zilizo katika mazingira magumu huku zikijiandaa kuanza mwezi mtukufu wa Ramadhan wiki ijayo.
Ramadhan ya mwaka huu, inayotarajiwa kuanza kati ya Februari 18 na 19, inakuja wakati ambapo maeneo kadhaa nchini yanakabiliwa na ukame.
Baadhi ya kaunti zilizoathirika ni Mandera, Turkana, Wajir, Garissa, Marsabit, Isiolo, Kajiado, Kilifi, Kwale, Lamu na Tana River.
Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Bw Wesley Koech, alisema hatua hiyo inalenga kupunguza mzigo wa kifedha kwa familia hizo wakati wa mwezi mtukufu.
“Lengo letu ni kuona wakitekeleza ibada ya mfungo kwa urahisi,” alisema Bw Koech.
Katika eneo lote la Pwani, maandalizi yanaendelea kwa kasi kuelekea Ramadhan.
Wafanyabiashara wanaongeza bidhaa madukani ili kuhakikisha waumini wanapata mahitaji yote muhimu, huku maafisa wa usalama pia wakiongeza ulinzi kutokana na shughuli nyingi zinazotarajiwa kuendelea hadi usiku wa manane na alfajiri.
Kamishna huyo wa Kaunti, alieleza kuwa kundi la kigaidi la Al-Shabaab huwa na mazoea ya kutekeleza mashambulizi kabla au mara tu baada ya Ramadhan kuanza.
“Hivyo basi, kama vyombo vya usalama, tumeimarisha hatua zetu kwa kuzingatia uangalizi mkali, doria zaidi na ukusanyaji wa taarifa za kijasusi ili kuhakikisha usalama wa umma wakati wote,” alisema Bw Koech.
Maafisa wa usalama katika kaunti za Mombasa, Kwale na Kilifi, ambako magenge ya vijana mara nyingi huleta vurugu wakati kama huu, pia walisema wameongeza juhudi za kiusalama.
Wiki iliyopita, Kamanda wa Polisi wa Ukanda wa Pwani, Bw Ali Nuno, aliwaagiza maafisa wa polisi kukabiliana vikali na wahalifu ambao hushambulia raia kwa panga.
Bw Mohamed Sharif, kiongozi wa Kiislamu katika eneo la Tudor, Kaunti ya Mombasa, alieleza wasiwasi kuhusu ongezeko la bei za bidhaa muhimu kila wakati Ramadhan inapokaribia.
“Serikali ina uwezo wa kudhibiti shughuli za wafanyabiashara hawa. Wanajua Ramadhan ni kipindi ambacho chakula na bidhaa muhimu hununuliwa kwa wingi,” alisema Bw Sharif.
Bi Raya Famau, kiongozi wa wanawake na mwanaharakati wa haki za binadamu katika Kaunti ya Lamu, alisema kupanda kwa bei ya bidhaa muhimu kama nafaka na mafuta ya kupikia kutafanya iwe vigumu kwa familia nyingi kuandaa mlo wa iftar na suhoor.
Mwenyekiti wa Baraza la Makasisi wa Dini Mbalimbali Pwani (CICC) Mohamed Abdulkadir, alitoa wito usaidizi utolewe kwa waumini wasiojiweza.