Habari

Serikali yazima upeperushaji wa moja kwa moja wa maandamano ya Juni 25

Na CHARLES WASONGA June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imezima upeperushaji wa matukio ya moja kwa moja ya maandamano ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu kuuawa kwa Gen Z wakipigania utawala bora.

Kwenye taarifa aliyoitoa mwendo was aa saba Juni 25, 2025, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Mawasiliano Nchini (CAK) David Mugonyi aliagiza redia na runinga za humu nchini kusitisha upeperushaji wa matukio ya maandamano mubashara.

“Upeperushaji wa maandamano ya Juni 25, 2025 ni kinyume na vipengele vya 33 (2) na 34 (1) vya Katiba na Sehemu ya 361 ya Sheria kuhusu Habari na Mawasiliano (CICA) ya 1998,” akasema Bw Mugonyi.

“Kwa hivyo, vituo vya televisheni na redio vyote vinaagizwa kusitisha upeperushaji wa maandamano moja kwa moja. Vituo vitakavyokiuka agizo hilo vitachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria ya Habari na Mawasiliano ya 1998,” akaongeza.

Kabla ya CAK kutoa agizo hilo, maandamano yalishuhudiwa katika zaidi ya kaunti 20 ambapo vijana walijitokeza kudai haki kwa waathiri wa maandamano ya Juni 25, 2024.

Maandamano hayo yaliitishwa kupigania utawala bora na kupinga Mswada wa Fedha wa 2024 uliosheheni mapendekezo ya kuongezwa kwa aina mbalimbali za ushuru.