Shirika lataka afisa achunguzwe kuhusu ushonaji wa sare za polisi
SHIRIKA moja lisilo la kiserikali lenye makao yake Mombasa, linamtaka Inspekta Jenerali wa Polisi kuchunguza afisa wa cheo cha juu wa polisi kwa madai kwamba alimwagiza fundi wa nguo eneo la Changamwe kumshonea sare za polisi kinyume cha kanuni za huduma ya polisi.
Kulingana na stakabadhi za kesi mahakamani, shirika la Centre for Litigation and Trust linadai kuwa Bw Samuel Kariuki, aliyekuwa Naibu Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Changamwe, alimwagiza Bw Mark Onyango Otweyo, kumshonea sare hizo.
Inadaiwa Bw Kariuki alimlipa fundi huyo Sh4,200 kwa kazi hiyo.
Shirika hilo linadai kuwa ili kuficha kosa hilo, afisa huyo alipanga kukamatwa kwa Bw Onyango na kumsingizia shtaka la kujipatia pesa kwa njia ya udanganyifu.
Stakabadhi za mashtaka zinaonyesha kuwa Bw Onyango alidaiwa kupokea fedha hizo Agosti 9, 2025, akijifanya ana uwezo wa kushona sare za polisi.
Mahakama ilimwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo, Bw Julius Ogogoh, kumkabidhi afisa huyo pamoja na Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga na Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) stakabadhi za kesi ambayo itatajwa Machi 18.
Bw Ogogoh alisema hakuna afisa aliye na mamlaka ya kumwagiza raia kushona sare za polisi bila idhini rasmi au bila kuidhinishwa.
Alionya kuwa kuruhusu raia wasioidhinishwa kushona sare za maafisa wa polisi kunahatarisha usalama kwa kuwa kunawapa watu wasiofaa fursa ya kupata mavazi na nembo rasmi za polisi, pamoja na hatari ya kughushi na kushuka kwa ubora.
Aidha, alisema DPP ana wajibu wa kikatiba kumwelekeza Inspekta Jenerali kuchunguza tuhuma zozote za uhalifu dhidi ya maafisa wa polisi, huku IPOA ikiwa na mamlaka ya kufanya uchunguzi huru kuhusu makosa ya jinai au kinidhamu yanayofanywa na wanachama wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi.