Sifuna asisitiza kuwa Ruto hastahili muhula wa pili uongozini
KATIBU Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, anaendelea kukosoa vikali utawala wa Kenya Kwanza unaoongozwa na Rais William Ruto, akisisitiza kuwa serikali hii inastahili muhula mmoja tu kwa kukosa uwezo wa kuongoza kutimiza matarajio ya wananchi.
Haya yanajiri huku akithibitisha tena kuwa chama cha ODM kimejipanga kuwania urais mwaka wa 2027, akisisitiza kuwa ODM inajiandaa kumenyania mamlaka na vyama vingine vya kisiasa.
Katika mahojiano ya kipekee na Taifa Leo, msemaji huyo wa ODM alibainisha kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho, ODM kila mara imekuwa na mgombeaji wa urais, wala haoni sababu yoyote ya uchaguzi ujao kuwa tofauti.
Ingawa alikiri umuhimu wa ushirikiano wa kisiasa, Bw Sifuna alisema kuwa chama hicho hapo awali kimewahi kushirikiana na washirika wenye mitazamo inayofanana, na kitawazia uwezekano wa kuunda miungano wakati ufaao ukifika.
Akizungumzia kuhusu jaribio la hivi karibuni la kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Muungano wa Afrika (AUC) la kiongozi wa ODM Raila Odinga bila mafanikio, Bw Sifuna alidai kuwa matokeo hayo hayaakisi uwezo wa Bw Odinga, bali yalikuwa kura ya maoni dhidi ya sera za kigeni za Rais Ruto, alizosema zimejaa makosa mengi na kushusha hadhi ya Kenya katika jukwaa la kimataifa.
Bw Sifuna pia alikosoa baadhi ya waliokuwa viongozi wa ODM walioko sasa katika serikali ya Kenya Kwanza, akisisitiza kuwa mawaziri hawapaswi kuwa na misimamo ya kisiasa ya upande wowote.
“Mawaziri wote wanahudumu kwa hisani ya Rais Ruto na wanatekeleza Ajenda ya Uchumi ya UDA—si sera ya ODM wala Azimio,” alisema.
Alisisitiza kuwa viongozi hao wamekana uaminifu wao kwa ODM kwa kujiunga na serikali, na hivyo wanapaswa kutazamwa na kupimwa kwa muktadha huo.
Baadhi ya waliokuwa viongozi wa ODM walioteuliwa kwenye baraza la mawaziri ni pamoja na Opiyo Wandayi (Nishati), John Mbadi (Hazina ya Kitaifa), Hassan Joho (Madini), Wycliffe Oparanya (Vyama vya Ushirika) na Beatrice Askul (Jumuiya ya Afrika Mashariki – EAC).
Bw Sifuna aliendelea kusisitiza haja ya uongozi wa maadili nchini, akihimiza viongozi kukumbatia siasa zisizokiuka maadili au zenye tamaa ya mali.
“Uongozi ni wito mkuu,” alisema.
“Ni lazima tukumbuke kuwa tupo hapa kwa msimu tu.”