Tanzania, Uganda zawekwa kwenye hatari ya kupigwa marufuku na Trump
SERIKALI ya Amerika inawazia kuzuia raia wa Tanzania, Uganda, DRC na Sudan Kusini miongoni mwa nchi 36 zaidi katika kile kitakuwa upanuzi mkubwa wa marufuku ya usafiri iliyotanganzwa na utawala wa Donald Trump mapema mwezi huu, kulingana na taarifa ya wizara husika.
Miongoni mwa orodha mpya ya nchi ambazo zinaweza kupigwa marufuku ni pamoja na washirika wakubwa wa Amerika kama vile Misri, Djibouti na mataifa ya Caribbean, Asia ya Kati na visiwa wa Pasifiki.
Hatua hiyo itakuwa upanuzi mkubwa wa sera ya utawala wa Trump ya kuzima wahamiaji.
Kwenye nakala hiyo iliyotiwa saini na Waziri wa Mashauri ya Kigeni Marco Rubio, na kutumwa Jumamosi kwa mabalozi wanaofanya kazi katika nchi husika, nchi hizo zilipewa siku 60 kuafikia vigezo vipya ambavyo wanastahili kuviweka lau sivyo nchi zao ziangukiwe na shoka.
Barua hiyo ilieleza vigezo ambavyo serikali ya Amerika inasema inahisi serikali husika haiziafikii katika suala la uhamiaji.
Baadhi ya nchi zilitajwa kuwa na ulaghai uliokithiri katika utoaji stakabadhi za usafiri huku zingine zikidaiwa kuruhusu idadi kubwa ya raia wao kusalia Amerika licha ya visa zao kuisha muda.
Nchi zingine zinazokabiliwa na marufuku ni: Angola; Antigua na Barbuda; Benin; Bhutan; Burkina Faso; Cabo Verde; Cambodia; Cameroon; Dominica; Ethiopia; Egypt; Gabon; Gambia; Ghana; Ivory Coast; Kyrgyzstan; Liberia; Malawi; Mauritania; Niger; Nigeria; Saint Kitts na Nevis; Saint Lucia; Sao Tome and Principe; Senegal; Syria; Tonga; Tuvalu; Vanuatu; Zambia; na Zimbabwe.
Wanasiasa wa Democrats na wakosoaji wengine wa Trump wamekashifu hatua ya kuzima wahamiaji haswa kwenye nchi maalum kama ubaguzi na kuifananisha na ile iliyowahi kutolewa dhidi ya mataifa ya Kiislamu.