Habari

Tumezima mtandao wa X kwa sababu umejaa ponografia, serikali ya Tanzania yafafanua

Na CHARLES WASONGA June 5th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Tanzania imeamua kuwazima raia wake kutumia mtandao wa kijamii wa X (zamani, twitter) kwa sababu unaruhusu usambazaji wa jumbe na picha za ngono, Waziri wa Habari Jerry Silaa amesema.

Usambazaji wa jumbe na picha chafu unaenda kinyume na “sheria, tamaduni na desturi za Tanzania,” waziri huyo akaambia runinga moja nchini humo.

Hatua hiyo imejiri baada ya Tanzania kudhibiti matumizi ya mtandao wa X majuma mawili yaliyopita kufuatia kupanda kwa taharuki ya kisiasa na kudukuliwa kwa akaunti ya X ya Jeshi la Polisi.

Lakini serikali haikuzima kabisa mtandao huo wa kijamii.

Kundi moja la kutetea haki nchini Tanzania lilisema agizo la Waziri Silaa linaakisi “mtindo wa kuchukiza wa ukandamizaji wa kimtandao” unaoendelezwa nchini huo kuelekea chaguzi za urais na ubunge zilizoratibiwa kufanyia Oktoba mwaka huu.

Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imelaumiwa kwa kuendeleza ukandamizaji na vitendo vingine vya ukiukaji wa haki inapojizatiti kusalia mamlakani.

Kwenye taarifa, shirika la Legal and Human Rights Centre (LHRC) lilisema mtandao wa X pia ulizimwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2020 na hivyo “kurejelewa kwa marufuku kama hiyo kunaibua hofu kuhusu nafasi ya uhuru wa mawasiliano mitandaoni nchini Tanzania.”

Apu nyingine maarufu kwa kutuma jumbe za sauti “Clubhouse” na ule wa kupitisha jumbe fupi, “Telegram” pia hazitumiki pasina matumizi ya mtandao wa Virtual Private Networks (VPN), shirika hilo la kutetea haki liliongeza.

LHRC ilisema inaudhi kwamba huku waziri Silaa akithibitisha kuwa serikali ndio imezima matumizi ya X, maafisa wa serikali na taasisi za umma zinaendelea kutumia mtandao huo.

“Hali hii inakanganya umma na inahujumu uhalalani agizo la serikali,” LHRC ikaongeza.

Kwenye mahojiano katika runinga, Waziri Silaa pia alihusisha marufuku hiyo na tangazo lilitolewa na X mwaka jana kwamba haitazuia usambazaji ‘content’ ya watu wazima iliyotengenezwa na kusambazwa kutokana na makubaliano baina ya wahusika.

Waziri huyo alinukuliwa akisema kuwa mtandao wa X umeruhusu “jumbe na picha za kingono, ikiwemo zile za watu wa jinsia moja  kinyume na mwongozo unaokubalika wa matumizi ya ngono nchini Tanzania.”

“Hata katika YouTube utagundua kuwa ni vugumu kupata baadhi ya picha na jumbe kama hizo. Kwa hivyo, hatua hiyo ni sehemu ya juhudi zetu za kulinda watumiaji wa mitandao ya kijamii na kuhakikisha kuwa majukwaa yote ya mitandao inayotumika nchini mwetu yanazingatia sheria zetu,” Silaa akasema.