Uhaba wa mafuta washuhudiwa nchini licha ya serikali kusisitiza kuna akiba ya kutosha
UHABA wa mafuta umeanza kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali nchini huku madereva wakiripoti kuyakosa vituoni, licha ya serikali kusisitiza akiba ya kitaifa bado iko thabiti.
Katika jiji la Nairobi, hasa kwenye Barabara ya Lang’ata, baadhi ya vituo vya mafuta vimeripotiwa kukosa kabisa petroli na dizeli na kuanza kuuza kwa vipimo.
Madereva wengi wamelazimika kuzunguka kutoka kituo kimoja hadi kingine wakitafuta mafuta, mara nyingi bila mafanikio.
“Nimelazimika kutembelea karibu vituo vitano vya mafuta. Hapa ndipo hatimaye nimepata mafuta, ingawa ni kidogo. Kuna uhaba mkubwa wa mafuta,” alisema Marvin Ogeta, dereva wa teksi aliyefanikiwa kupata mafuta katika kituo kimoja kwenye barabara hiyo.
Mhudumu katika kituo kingine alisema petroli ilikuwa imeisha huku dizeli pekee ikibaki, akiongeza kuwa shehena mpya ya mafuta ilitarajiwa lakini hakuwa na uhakika wa lini itawasili.
Hali hiyo imewalazimu madereva kubadili ratiba zao za kazi kwa kupunguza safari na kuendesha kwa tahadhari zaidi.
“Madereva wanalazimika kupunguza safari na kuhesabu vizuri matumizi ya mafuta ili mwishoni mwa siku mapato yawe na maana,” alisema Jon Mutua, dereva na mkazi wa Karen.
Hata hivyo, Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi amesema usambazaji wa mafuta nchini bado uko thabiti, akieleza kuwa mpango wa uagizaji mafuta kati ya serikali na serikali bado unaendelea licha ya misukosuko Mashariki ya Kati.
Katika eneo la North Rift, uhaba huo unaonekana kuwa mkubwa zaidi.
Miji kama Eldoret, Kitale, Kapsabet, Bungoma na sehemu za Pokot Magharibi upungufu wa dizeli umeripotiwa huku baadhi ya vituo vikimaliza kabisa akiba yao.
Hali hiyo imeathiri wakulima walio katikati ya msimu wa upanzi kwani wengi hutegemea mashine zinazotumia dizeli.