Habari

Ukraine yageuka kichinjio kwa Wakenya wanaoajiriwa na jeshi la Urusi 4 wakiuawa

Na RUTH MBULA February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIILI ya raia wawili zaidi wa Kenya waliokuwa wameajiriwa kama wanajeshi wa Urusi imepatikana katika mji wa Lyman, eneo la Donetsk nchini Ukraine.
Idara ya Ujasusi wa Ulinzi ya Ukraine, yenye jukumu la kulinda usalama wa taifa hilo, iliripoti Ijumaa, Februari 6, 2026 kuwa Wakenya hao ni Ombwori Denis Bagaka aliyezaliwa Januari 30, 1987 na Wahome Simon Gititu aliyezaliwa Mei 21, 1991.
Miili yao ilipatikana karibu na mwili wa Mkenya mwingine, Clinton Nyapara Mogesa, ambaye kifo chake kilitangazwa Januari 31, 2026 na maafisa wa Ukraine.
Nyapara, mwenye umri wa miaka 29, alitoka kijiji cha Riateri katika eneo la Bonchari, Kaunti ya Kisii.
Familia yake ilisema alikuwa akiishi na kufanya kazi nchini Qatar kabla ya kutia saini mkataba na majeshi ya Shirikisho la Urusi na kupelekwa katika kikosi cha mashambulizi cha jeshi hilo.
Wakati mwili wa Nyapara ulipopatikana, mamlaka za Ukraine ziliripoti kuwa alikuwa na pasipoti za raia wengine wawili wa Kenya.
Wakenya wote watatu; Bagaka, Gititu na Nyapara wanadaiwa kushawishiwa kujiunga na vita vya Urusi dhidi ya Ukraine walipokuwa nchini Qatar.
Bagaka na Nyapara waliwasili katika kituo cha usajili mjini Yaroslavl Septemba 27, 2025, huku Gititu akijiunga nao mwezi mmoja baadaye, Oktoba 28.
“Kiongozi mkuu katika kuwasafirisha Wakenya hawa hadi kwenye vifo vyao alikuwa raia wa Kyrgyzstan aitwaye Salizhan Uulu Almamet, aliyekuwa akiwakilisha mamluki wa Urusi. Almamet alitia saini mikataba na jeshi la Urusi kwa niaba ya Bagaka, Gititu na Nyapara huko Yaroslavl, na pia akadhibiti akaunti zao za benki,” iliripoti Idara ya Ujasusi wa Ulinzi ya Ukraine.
Kutoka Yaroslavl, Wakenya hao waliripotiwa kupelekwa katika uwanja wa mafunzo wa Pogonovo karibu na Voronezh, hasa katika kitengo cha kijeshi nambari 11097.
Uwanja huo hutumiwa na Urusi kutoa mafunzo ya haraka ya kijeshi, ambapo waajiriwa hutumwa moja kwa moja kwenye vikosi vinavyopigana Ukraine.
Ndani ya kitengo hicho cha kijeshi, kuna kile kinachoitwa “kikosi cha adhabu”, ambacho hujumuisha wafungwa, waliotoroka jeshini, walevi sugu, waraibu wa dawa za kulevya na mamluki wa kigeni.
Bagaka, Gititu na Nyapara walijikuta katika kikosi hicho, ambacho kwa mujibu wa ushahidi wa wanajeshi wa Urusi waliotekwa, hutumiwa kwa oparesheni za kivita.
Baada ya kipindi kifupi cha mafunzo, Wakenya hao watatu walitumwa Donbas kuvamia mji wa Lyman. Walipokuwa wakipitia eneo linaloitwa ‘eneo la mauaji’, majeshi ya ulinzi ya Ukraine yaliwaangamiza mamluki wote watatu, pambano lao la kwanza likawa la mwisho,” mamlaka za Ukraine zilisema.
Inasemekana kuwa miili ya Wakenya hao watatu haikuondolewa kutoka uwanja wa vita.
“Idara ya Ujasusi wa Ulinzi ya Ukraine inaendelea kurekodi visa vya raia wa kigeni kuajiriwa katika jeshi la Urusi,” iliongeza taarifa hiyo.
Vifo vya Wakenya hao watatu vinajiri kuwa na ongezeko la ripoti kuhusu Waafrika wengi kuajiriwa kujiunga na vita vya Ukraine, wakivutiwa na ahadi za kazi nzuri, mapato ya haraka au uraia.
Kuna hofu kuwa baadhi yao waliishia kujiunga na jeshi bila kufahamu baada ya kuwasili Urusi kwa madai ya ajira za kiraia.
Wizara ya Masuala ya Kigeni na Masuala ya Wakenya Ughaibuni imethibitisha kupokea simu za dharura kutoka kwa Wakenya waliokwama au kunaswa Urusi.