UNOC3: Guterres asihi mataifa kuokoa bahari ili ajira zisipotee
KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bw António Guterres ametoa mwito kwa mataifa kujitahidi kukabiliana na masuala yanayoathiri afya ya baharini, ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa taka za plastiki na shughuli zingine haramu.
Akizungumza katika kikao na wanahabari katika Makala ya Tatu ya Kongamano la Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya baharini (UNOC3) jijini Nice, Ufaransa, Bw Guterres aliangazia umuhimu wa bahari katika kuhimili uhai na maisha ya wakazi wa mataifa yenye fuo kama vile Kenya.
“Bahari ni moyo wa ulimwengu,” alisema, huku akiukumbusha ulimwengu kwamba bahari inasaidia kuunda nafasi nyingi za ajira, huku wakazi wengi wa maeneo ya pwani wakitegemea rasilimali hii.
“Lakini licha ya umuhimu wa bahari, tunaendelea kutumia rasilimali hii vibaya bila kujali kuwepo kwa athari za baadaye.”
Hapa nchini, pwani ya Kenya inayokadiriwa kuwa ya urefu wa kilomita 600 kwenye ufuo wa bahari ya Hindi, ni muhimu kwa maisha ya mamilioni ya watu kupitia uvuvi, utalii na biashara kwa njia ya baharini.
Hata hivyo, nchi hii imekuwa ikikumbwa na changamoto kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi, kuongezeka kwa viwango vya maji ya bahari, uchafuzi unaotokana na taka za plastiki na shughuli haramu za uvuvi.
SOMA PIA: Kongamano la uchumi wa baharini laanza Ufaransa Macron akiisuta Amerika
Kenya imekuwa ikishuhudia hasara kiuchumi kutokana na uvuvi haramu. Shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo (FAO) linakadiria kwamba uvuvi haramu huzigharimu nchi zinazostawi kufikia $10 bilioni kila mwaka, huku Kenya ikiwa miongoni mwa mataifa yaliyoathirika pakubwa katika eneo la Afrika Mashariki.
Bw Guterres alipongeza ufanisi wa hivi karibuni ambao umeshuhudiwa kimataifa, ikiwa ni pamoja na Mapatano ya Umoja wa Mataifa kuhusiana na Sheria za Baharini (UNCLOS), pamoja na makubaliano ya kihistoria ya ulinzi wa mazingira na uhai wa baharini mbali na himaya za kitaifa (BBNJ), ambapo Kenya ni mojawapo ya mataifa ambayo yametia saini kuidhinisha.
Huku akijibu maswali kutoka kwa wanahabari kuhusu ulinzi wa samaki kutokana na uvuvi haramu, tatizo ambalo linakumba mataifa yanayoendelea hasa ikizingatiwa hayana uwezo wa kujilinda, Bw Guterres alikiri mchangamoto zinazoyakumba mataifa kama vile Kenya.
Aliahidi kwamba shirika hilo litaimarisha mifumo ya uwajibikaji na kuimarisha ushirikiano, ili kukabiliana na uvuvi haramu, shughuli ambazo zinahatarisha uhai baharini.
Kuhusu changamoto ya uchafuzi wa mazingira ya baharini, Bw Guterres alisisitiza haja ya kuwepo kwa mkataba wa kimatifa kusitisha matumizi ya plastiki.
“Kupiga marufuku matumizi ya bidhaa za plastiki zinazoitumika mara moja ni muhimu,” alisema.
Aidha, alisema kwamba ili kufikia azimio la kulinda asilimia 30 ya uhai wa baharini na maeneo ya pwani kufikia mwaka wa 2030, lazima kuwe na ushirikiano kuhakikisha kwamba sheria zinafuatwa.
Alitoa mwito kwa mataifa kutoa mipango yao thabiti ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika kongamano la kimataifa kuhusu masuala ya mabadiliko ya tabianchi COP 30, linalopangiwa kufanyika mwisho wa mwaka huu nchini Brazil.
Makala haya yametayarishwa kupitia usaidizi wa Association Africa21