Habari

Ushindi wa Atwoli kuongoza Cotu kwa muhula wa sita wapingwa kortini

Na JOSEPH WANGUI March 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUCHAGULIWA tena kwa Francis Atwoli kama Katibu Mkuu wa COTU-K kumepingwa mahakamani kwa madai kuwa, mchakato wa uchaguzi ulikiuka sheria zinazosimamia uchaguzi wa vyama vya wafanyakazi.

Walalamishi wawili, Fazul Mahamed na taasisi ya Institute for Democratic Governance, wanadai kuwa kura hiyo ilifanyika mapema kabla ya muda unaoruhusiwa kisheria katika mzunguko wa uchaguzi wa vyama vya wafanyakazi.

Katika kesi iliyowasilishwa katika Mahakama ya Ajira na Leba jijini Nairobi, walalamishi wanataka mahakama ibatilishe matokeo ya uchaguzi uliofanyika Machi 14 wakati wa mkutano wa wajumbe wa baraza tawala la COTU uliofanyika Kisumu.

Katika uchaguzi huo, Bw Atwoli alichaguliwa bila kupingwa kuhudumu muhula wa sita kama Katibu Mkuu wa muungano huo wa vyama vya wafanyakazi.

Hata hivyo, walalamishi wanasema uchaguzi huo ulifanyika kabla ya kuanza rasmi kwa awamu ya uchaguzi wa kitaifa wa vyama vya wafanyakazi, na hivyo uchaguzi wa Bw Atwoli hauwezi kutambuliwa kisheria.

Wanadai kuwa Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi alikuwa tayari ametoa waraka ulioeleza ratiba rasmi ya mzunguko wa uchaguzi wa vyama vya wafanyakazi wa 2026.