Ushuhuda wa mtoto watumiwa kumfunga mshukiwa wa unajisi
UAMUZI wa Mahakama Kuu mjini Malindi umemulika sheria kuhusu uzito wa ushahidi wa watoto katika kesi za makosa ya kingono, wakati ushahidi mwingine hauridhishi.
Hali hii ilijitokeza wakati mahakama ilipokuwa ikipitia hukumu ya kifungo cha miaka 30 iliyotolewa dhidi ya mwanamume aliyekuwa amemuoa msichana wa miaka 15.
Mwanamume huyo alikamatwa baada ya maafisa wa polisi kuvuruga sherehe iliyokuwa inalenga kuhalalisha ndoa hiyo, kati ya Mei 1 na Mei 20, 2022, katika Kaunti Ndogo ya Kaloleni, Kaunti ya Kilifi.
Mahakama ilibainisha kuwa, ushahidi wa kimatibabu uliokuwepo haukuunga mkono madai ya unajisi.
Mahakama ilidumisha hatia ya Baraka Kaingu kwa kosa la kunajisi mtoto, lakini ilipunguza adhabu iliyotolewa na mahakama ya chini kutoka miaka 30 hadi kifungo cha miaka 20 jela, ambayo ni adhabu ya juu zaidi kwa kosa kama hilo.
Katika uamuzi wake, Mahakama Kuu ilisema Kaingu alipaswa kuchukuliwa kama mkosaji wa mara ya kwanza kwa kuwa hakukuwa na ushahidi wa makosa ya awali.
Mahakama ilitumia sheria inayoruhusu kutoa hukumu kwa kuzingatia ushahidi wa mtoto pekee iwapo mahakama inaamini kuwa mtoto huyo anasema ukweli.