Habari

Uzinduzi wa chama cha DCP wahairishwa hadi mwisho wa mwezi huu

Na WINNIE ONYANDO June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

UZINDUZI wa chama cha aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua cha Democracy for the Citizens (DCP) uliopangwa kufanyika Juni 3, 2025 umehairishwa tena.

Chama hicho sasa kitazinduliwa rasmi mwisho wa mwezi huu.

Hii ni baada ya uongozi wa chama hicho kushindwa kupata ukumbi wa kuandaa hafla hiyo.

“Uzinduzi wa chama sasa utafanyika katika ukumbi wa faragha” chama hicho kilisema.

Hapo awali, Bw Gachagua alisema kuwa chama hicho kingezinduliwa Juni 3, 2025.

Tarehe hiyo ilifichuliwa katika barua ambayo chama kiliomba kutumia Ukumbi wa Uwanja wa Michezo wa Kasarani kwa hafla hiyo.

Ombi hilo lililowasilishwa Mei 20, lilionyesha maandalizi ya kina yaliyofanywa ili kuhakikisha mafanikio ya tukio hilo.

“Ninaandika kuomba rasmi kutumia Ukumbi wa Kasarani Gymnassium kwa uzinduzi rasmi wa chama chetu, unaopangwa kufanyika Jumanne, Juni 3, 2025, kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi na moja jioni,”  ilisema sehemu ya barua hiyo.

“Hafla hiyo inatarajiwa kuhudhuriwa na watu takriban 5,000, wakiwemo wanachama wa chama, wafuasi, wageni waalikwa, na wanahabari,” iliendelea.

Hata hivyo, chama hicho Juni 4, 2025 kilisema kuwa serikali imekataa ombi lao la kutaka kutumia ukumbi huo wa Kasarani.