Vijana wafika jijini kuandamana licha ya usalama kuimarishwa
USALAMA umeimarishwa vikali katika jiji la Nairobi kuanzia asubuhi Jumatano Juni 25, huku maafisa wa polisi wakifunga barabara kuu zinazoelekea katikati ya jiji (CBD), katika maandalizi ya maandamano yanayoendelea. Hali hii ilibabisha usumbufu mkubwa kwa waliotaka kufika katikati ya jiji.
Hata hivyo, vijana wamefaulu kufika kati kati ya jiji na kuanza maandamano huku maduka yakifungwa na magari yakiwa machache sana.
Polisi waliweka vizuizi na kuanza kukagua magari, huku wakidhibiti kabisa yanayoingia katikati ya jiji. Magari ya usafiri wa umma yaliathiriwa zaidi, na abiria kulazimika kushuka mbali na katikati ya jiji na kutembea kwa miguu.
Barabara za Parliament Road, Harambee Avenue na Kenyatta Avenue zilifungwa kabisa, na maafisa wa usalama wameweka waya wa miiba pamoja na vizuizi vingine. Maandamano haya ni kumbukumbu ya hali iliyoshuhudiwa wakati wa maandamano Juni 25 mwaka jana.
Matatu kutoka barabara ya Mombasa zililazimika kusimama katika makutano ya Haile Selassie Avenue na Uhuru Highway huku za kutoka Thika Road zikiishia Guru Nanak.
Matatu kutoka Jogoo Road ziliishia City Stadium, huku usalama ukiwa mkali karibu na maeneo muhimu ya serikali. Barabara zinazoelekea Ikulu pia zilifungwa.
Hali ilikuwa shwari barabara ya Thika asubuhi kabla ya kuziuzi kuwekwa karibu na hospitali ya Guru Nanak
Waziri wa Usalama wa Ndani na Utawala wa Kitaifa, Kipchumba Murkomen, alitembelea katikati ya jiji la Nairobi, huku idara za usalama zikiongeza doria.
Akiandamana na Naibu Mkuu wa Polisi, Gilbert Masengeli, Murkomen alitembea hadi Jogoo House A kukutana na Mkuu wa Polisi, Douglas Kanja.
Kabla ya mkutano huo, Waziri Murkomen alitembelea Harambee House ambako alizungumza na maafisa wa usalama waliokuwa kazini. Pia alikutana kwa kifupi na maafisa waliokuwa wakilinda usalama barabarani, na kuzungumza na wakazi wa Nairobi waliokuwa wakielekea kazini.
Biashara nyingi zilikuwa zimefungwa. Maandamano yanaendelea katikati ya jiji la Mombasa.