Habari

Vijana watatiza usomaji wa hotuba ya Rais katika Madaraka Dei ugani Gusii

Na WYCLIFFE NYABERI  June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 1

BAADHI ya vijana waliohudhuria sherehe za Madaraka Dei katika kaunti ya Kisii walitatiza kwa muda usomaji wa hotuba ya Rais William Ruto.
Sherehe za kaunti hiyo ziliandaliwa ugani Gusii na zilijaa mbwembwe na doido tangu kuanza kwake.
Lakini ilipotimia zamu ya kamishina wa kaunti ya Kisii Joseph Kibet kuisoma hotuba ya rais William Ruto kama ilivyo kawaida wakati wa hafla kama hizo, vijana hao walianza kupiga kelele.
Vijana hao walikuwa wameketi katika jukwaa la G6, ambalo ni maarufu sana kwa visa vya uhuni ugani humo.
Wakirukaruka na kurusha chupa za maji hewani, vijana hao walitoa kauli za “Ruto Must Go” huku wengine wakitoa kibwagizo cha “One Term”.
Gavana wa Kisii Simba Arati alipoona kelele hizo zinakolea, aliingilia kati na kuuliza vijana hao wamruhusu kamishina akamilishe usomaji wa hotuba ndefu ya rais.
“Tafadhali vijana, ruhusuni kamishina wa kaunti atamatishe kusoma hotuba ya rais,” mbunge huyo wa zamani wa Dagoretti Kaskazini alisema.
Vijana hao hawakutii agizo hilo la gavana na waliendelea kupiga kelele zao.
Alipomaliza kuisoma hotuba ya rais, Bw Kibet alisema, “naona kuna watu wachache waliochoka. Lakini hivyo ndivyo maisha yalivyo.”