Viongozi wa ODM: Hata mtuambie nini, kwa serikali hatutoki ng’o!
VIONGOZI wa ODM wamekariri kujitolea kwao kuunga mkono utawala wa Rais William Ruto, wakisema ndio njia ya kipekee ya kuliwezesha eneo la Nyanza kupata maendeleo.
Mwenyekiti wa Kitaifa Gladys Wanga, Kiranja wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Millie Odhiambo na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Homa Bay Joyce Osogo walisema wako tayari kuhakikisha rais anatimiza mipango yake ya maendeleo kwa manufaa ya eneo hilo.
Lakini viongozi hao pia walisema wako tayari kuikosoa serikali endapo haitashughulikia changamoto nyingine
Chama cha ODM kilitia saini mkataba wa ushirikiano na UDA na kupelekea kuundwa kwa serikali jumuishi.
Kutokana na ushirikiano huo, Rais Ruto sasa anaweza kuzuru maeneo kadhaa ya Nyanza bila kukumbana na upinzani kutoka kwa viongozi na raia tofauti na siku za nyuma ambapo viongozi na wafuasi wao walichelea kufika katika mikutano yake.
Bi Wanga aliwahimiza wakazi kuendelea kuunga mkono ukuruba wa kisiasa kati ya kiongozi wa ODM Raila Odinga na Rais Ruto ili eneo hilo lifaidi kwa miradi ya maendeleo.
“Kuna afua mbili pekee kwa wakazi wa eneo hili. Kusalia serikalini na kushinikiza mgao mkubwa wa fedha za maendeleo au kuendeleza shinikizo hizo kupitia maandamano, mbinu ambayo haijazaa matunda,” Gavana huyo wa Homa Bay akaeleza.
“Tumefanya uamuzi wa kisiasa wa kusalia ndani ya serikali jumuishi kutuwezesha kupata rasilimali zaidi za kuwasaidia watu wetu. Tutafuata mkataba wa ushirikiano ambao Raila Odinga na Rais waliutia saini,” akasema.
Bi Wanga alisema chama cha ODM kimekuwa kikishinikizwa kujiunga na maandamano ya kuikashifu serikali kutokana na makosa mbalimbali kama vile ukatili wa polisi na maauji ya kiholela.
Hata hivyo, alisema chama hicho kitatumia mbinu za mazungumzo kuiwekea serikali presha ishughulikie masuala hayo “wala siyo mbinu ya maandamano.”
“Hatuwezi kushiriki maandamano ambayo yatailemaza serikali,” akaeleza Bi Wanga.
Kwa upande wake Bi Odhiambo alisema eneo bunge lake la Suba Kaskazini limefaidi kutokana na serikali kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya miundo msingi.
Kiranja huyo wa wachache katika Bunge la Kitaifa alitaja ujenzi wa barabara ya Pembeni ya Rusinga, kama moja kati ya miradi inayotekelezwa na serikali ya Rais Ruto katika eneo bunge la Suba Kaskazini.