Viongozi wamuomboleza nyota wa fasihi Profesa Ngũgĩ wa Thiong’o
RAIS William Ruto Alhamisi aliongoza taifa kuomboleza nyota wa fasihi Profesa Ngũgĩ wa Thiong’o, anayeheshimiwa na wengi kama mmoja wa waandishi mashuhuri zaidi Afrika.
Profesa huyo aliaga dunia siku ya Jumatano (Mei 28 2025) akiwa na umri wa miaka 87.
Akimtaja kama mwalimu mpendwa, mwandishi, na mtunzi wa michezo ya kuigiza, Rais Ruto alisema Profesa Ngũgĩ “ameacha alama ya kudumu katika tunavyotafakari kuhusu uhuru wetu, haki ya kijamii, pamoja na matumizi mabaya ta mamlaka ya kisiasa na kiuchumi.”
“Katika taaluma yake ya ujasiri na ubunifu, Profesa Ngũgĩ alitufundisha jinsi ya kutoa mchango usioweza kupuuzwa na kuzungumza kwa namna ambayo hata wapinzani walilazimika kusikiliza. Uzalendo wake haupingiki, na hata waliotofautiana naye walikiri kuwa hoja zake zilitokana na tamaa ya dhati ya ukweli na uelewa, si chuki wala dharau,” alisema Rais Ruto.
Aligusia suala la Tuzo ya Nobel ya Fasihi, ambayo mara nyingi ilisemekana anastahili kupokea, lakini hakuwahi kupewa.
“Wakenya wengi wanakumbuka wakati ambapo hatukuwa na matumaini kwamba Profesa Ngũgĩ angepokea Tuzo ya Nobel. Ingawa hakuwahi kupewa rasmi, atabaki kuwa shujaa wa ukombozi na ubunifu wa kifasihi mioyoni mwetu,” alisema Rais Ruto.
Profesa Ngũgĩ alifariki dunia nchini Anmerika baada ya kuugua kwa muda mrefu, kama ilivyothibitishwa na familia.
Mwanawe, Mukoma Ngũgĩ, ambaye pia ni mwandishi na msomi, alisema:
“Nampenda. Sijui kesho itakuwaje bila yeye.”
Binti yake, Wanjikũ Ngũgĩ, alisema baba yao aliishi maisha ya utimilifu na akawaomba Wakenya na jamii ya fasihi ulimwenguni kusherehekea maisha na kazi zake.
Naibu Rais Kithure Kindiki alimtaja Profesa Ngũgĩ kama mmoja wa wasomi bora wa Kenya ambaye aliheshimika hata na wale waliotofautiana naye.
Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen, alisema marehemu aliweka Kenya na Afrika kwenye ramani ya dunia kupitia kazi zake.
Kiongozi wa ODM Raila Odinga alisema kwa kifupi:“Shujaa wa Kiafrika ameanguka. Pumzika kwa Amani ya Milele, Profesa Ngũgĩ wa Thiong’o!”
Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi, alimkumbuka kama gwiji aliyeangaza Afrika Mashariki kupitia kazi kama The River Between, Petals of Blood na A Grain of Wheat ambazo zilieleza roho ya taifa.
Kiongozi wa chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka, alimtaja marehemu kama akili ya kipekee na mmoja wa waandishi bora duniani. AliyekuwaNaibu Rais Rigathi Gachagua alisema Afrika imebaki yatima baada ya kifo cha Profesa huyo, akimtaja kama mwalimu, mshairi, mwandishi hodari na mtu mwaminifu aliyebobea katika ulimwengu wa kifasihi.
Spika wa Bunge la Taifa Moses Wetang’ula alisema kazi ya Profesa Ngũgĩ haikuwa hadithi tu, bali ni vitendo vya uasi vilivyoakisi hadhi ya watu wa Afrika.
Spika wa Seneti Amason Kingi alimtaja kama fikra muhimu katika mapambano dhidi ya ukoloni wa lugha, akisema msimamo wake utaendelea kuathiri tafiti na harakati kwa vizazi vijavyo.
Kiongozi wa PLP Martha Karua alimtaja kama mzalendo aliyetoa mchango wa kipekee katika uelewa wa taifa la Kenya.
Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya alisema Profesa Ngũgĩ alibadili taswira ya utambulisho wa Mwafrika.
Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir alimkumbuka kama mlezi wa utamaduni aliyepambana na fikra za kikoloni na kurejesha simulizi za Kiafrika