Viongozi wataka padri aliyeuawa awe ‘kafara ya mwisho’ ya kutokomeza ujangili
MAGAVANA na viongozi wa kidini wamesema kwamba Padre Allois Bett, aliyeuawa akiwa katika harakati za kuhuhiri amani Tot, Bonde la Kerio wiki iliyopita, anapaswa kuwa “kafara ya mwisho” katika juhudi za kurejesha amani katika eneo la Kaskazini mwa Bonde la Ufa.
Wakizungumza wakati wa misa ya kumkumbuka padre huyo aliyeuawa, viongozi hao walielezea masikitiko yao kwamba licha ya serikali kuwekeza fedha nyingi katika kupambana na wizi wa mifugo na ujahili, eneo hilo linaendelea kushuhudia ghasia.
Katika ibada hiyo iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Moyo Mtakatifu wa Yesu mjini Eldoret, wanasiasa walilaani vikali vitendo vya ujangili wakivitaja kama aibu kwa taifa.
“Kama mtoto wa Bonde la Kerio na gavana wa eneo kulikotokea tukio hili, nimehuzunika sana, na hii aibu kwetu. Hata hivyo, haifai kutumia tukio hili kuhukumu jamii nzima, bali wale waliohusika lazima wakamatwe mara moja,” alisema Gavana wa Elgeyo Marakwet, Wisley Rotich.
Gavana Rotich alisema tangu tukio hilo litokee, wenyeji wamekuwa wakikutana ili kubaini wahalifu waliomuua padre huyo, kwa lengo la kufichua wote waliohusika.
“Jana, jamii ilituambia tuwape siku tatu pekee na watatupatia majina ya wahusika ili haki iweze kutendeka,” alisema Bw Rotich.
Aliwataka viongozi wa dini kuwaombea wakazi wa Bonde la Kerio, akisema hakuna mtu aliye salama katika eneo hilo.Alieleza kuwa hata viongozi wa kisiasa kutoka eneo hilo wako hatarini kutokana na hali ya usalama.
“Waombeeni wakazi wote wa Bonde la Kerio, hata mimi kwa sasa siko salama,” alisema. Gavana wa Nandi, Stephen Sang, aliunga mkono kauli ya mwenzake wa Elgeyo Marakwet, akisema ni wakati wa kuchukua hatua badala ya maneno mengi yasiyo na matokeo.
“Ni wazi kuwa maneno hayasaidii. Hali ya usalama katika Elgeyo Marakwet, hasa Bonde la Kerio, ni tata sana na mtu wa nje hawezi kuelewa kwa urahisi,” alisema Bw Sang.
Aliongeza kuwa hali hiyo ya ukosefu wa usalama imepelekea vifo vya watu wengi kutokana na ujangili na wizi wa mifugo. Alielezea masikitiko kuwa hata mabalozi wa amani kama vile marehemu padre, watoto na akina mama hawajasazwa na mauaji hayo.
“Watoto, akina mama, na hata mabalozi wa amani wameuawa. Kadri muda unavyosonga, wahalifu wameendelea kuvuka mipaka ya utu. Padre aliuawa akiwa kazini. Tumeunda kamati, kutoa maazimio na mijadala, lakini kila mara mipaka imevukwa. Hili la padre linapaswa kuwa la mwisho,” alisema Bw Sang.
Alisema sababu kuu ya ukosefu wa usalama katika eneo hilo ni ukosefu wa maendeleo, akibainisha kuwa limekuwa likisahaulika kwa muda mrefu.
“Jamii za eneo hilo zimeeleza wazi kuwa moja ya sababu ya hali hiyo ni kusahaulika kimaendeleo,” alisema. Hata hivyo, alilalamikia kwamba pesa nyingi zinazotolewa na serikali kwa eneo hilo ni kwa masuala ya usalama badala ya maendeleo.
Alisema wakati umefika kwa pesa hizo kuelekezwa katika miradi ya maendeleo na uwezeshaji wa kiuchumi.
“Serikali imekuwa ikituma fedha nyingi kwa usalama, lakini si kwa maendeleo. Tunataka fedha hizo zielekezwe katika miradi ya maendeleo ili kukomesha visa vya ukosefu wa usalama,” aliongeza Bw Sang.
Gavana wa Uasin Gishu, Jonathan Bii, alisema ni uchungu na jambo la kusikitisha kwamba padre aliyejitolea katika kazi ya umishonari aliuawa kwa njia ya kikatili.
Alimtaja marehemu kama mtumishi mwaminifu wa Mungu ambaye hakustahili kufa kwa njia hiyo.
Askofu wa Dayosisi ya Katoliki ya Eldoret,Dominic Kimengich, alisema kuuawa kwa Padre Bett ni mwito kwa serikali kuchukua hatua za kulinda Wakenya wote.
“Damu ya padre wetu Allois iwe muhuri wa amani ya kudumu Bonde la Kerio na Kenya kwa ujumla. Tunaomba serikali ichukue hatua na kurejesha utulivu katika eneo hilo,” alisema Askofu Kimengich.
Padre marehemu atazikwa Ijumaa, Mei 30.