Vuta nikuvute ndani ya chama cha DCP
VITA vya ndani vimezuka katika chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) kuhusu jinsi viongozi wake wakuu wanavyowakaribisha wanachama wapya katika kaunti mbalimbali za eneo la Mlima Kenya.
Mvutano huo unahusisha kiongozi wa chama Rigathi Gachagua na naibu wake Cleophas Malala, huku wanasiasa wengine ndani ya chama hicho wakirushiana lawama.
Mzozo huo umechochewa pia na chama cha Jubilee Party, kinachoongozwa na Rais (Mstaafu)Uhuru Kenyatta, ambacho kinamshutumu Gachagua kwa “kukimeza” kisiasa katika eneo la Mlima Kenya.
Kundi la wagombeaji wa Jubilee, linaloongozwa na aliyekuwa Mbunge wa Nyeri Mjini Ngunjiri Wambugu, limeandika barua kwa Kenyatta likitaka chama hicho kisalie huru na kijiandae kivyake kwa uchaguzi mkuu wa 2027 badala ya kushirikiana na DCP.
Mvutano huo umeibuka huku baadhi ya wanasiasa waliokuwa wakiunga mkono DCP, akiwemo Mbunge wa Githunguri Gathoni Wamuchomba, Mbunge wa Juja, George Koimburi na Mbunge wa Maragua, Mary Wa Maua, wakirudi katika chama cha United Democratic Alliance (UDA) kinachoongozwa na Rais William Ruto.
Mnamo Alhamisi, Machi 12, 2026, mwakilishi wa wanawake wa Kirinyaga Njeri Maina alimshambulia vikali Bw Malala akimlaumu kwa kuendesha njama za ndani za kukidhoofisha chama.
Malumbano kati yao yanadaiwa kuanza baada ya Malala kukutana na baadhi ya madiwani wa Kirinyaga katika hoteli moja kaunti ya Murang’a.
Maina alidai mkutano huo ulilenga kuunda kundi pinzani ndani ya DCP ili kumpinga Gachagua. Pia, alimshutumu Malala kwa kupokea fedha kutoka kwa watu wanaotaka kuvuruga ajenda ya chama na juhudi za kuunda serikali mbadala.
Hata hivyo, Malala alikanusha madai hayo akisema mkutano huo ulikuwa maandalizi ya kikao cha madiwani hao na Gachagua. Alisema lengo lao ni kupanua ushiriki wa kisiasa wanapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao.
Mkuu wa mikakati wa DCP Peter Mbae pia alimtetea Malala akisema mkutano huo ulikuwa na baraka za uongozi wa chama.
Kulingana naye, Gachagua alimpa Malala jukumu la kuwafikia viongozi na wanachama wapya wengi inavyowezekana.
Baadaye siku hiyo, Gachagua aliwakaribisha madiwani waliokutana na Malala nyumbani kwake Wamunyoro na kusisitiza kuwa wanaunga mkono DCP kwa maagizo ya wapiga kura wao.
Alisema madiwani hao wanataka kuwa watetezi wa jamii ya Mlima Kenya dhidi ya wale wanaodaiwa kuwanyanyasa kisiasa.
Gachagua pia aliahidi kufanya ziara ya siku tatu Kirinyaga kuwapigia debe wagombeaji wa DCP ili kuimarisha umaarufu wao.
Alisema analenga kuhakikisha chama hicho kinapata uungwaji mkono mkubwa katika mabunge ya kaunti za Mlima Kenya.
Kwa sasa, wachambuzi wa siasa wanaona mabadiliko hayo ya uungwaji mkono Kirinyaga kama pigo kwa gavana Anne Waiguru, ambaye ameonyesha nia ya kutoa mwelekeo wa kisiasa wa Mlima Kenya kuelekea uchaguzi wa 2027.
Gachagua, kwa upande wake, anaamini hatua ya wanasiasa wa UDA kuelekea DCP ni mwanzo tu wa mwelekeo mpya wa kisiasa katika eneo hilo huku maandalizi ya uchaguzi wa 2027 yakizidi kushika kasi.