Habari

Wabunge- Maandamano yalichochewa na ukosefu wa ajira, sio Gachagua

Na CHARLES WASONGA June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

WABUNGE wa mrengo wa upinzani Ijumaa Juni 27, 2025 waliendelea kumtetea aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua dhidi ya madai kuwa ndiye aliyewafadhili wahuni waliopora na kuharibu mali wakati wa maandamano ya Jumatano.

Wakiongozwa na naibu kiongozi wa wachache bungeni Robert Mbui wamtaka Rais William Ruto kushughulikia kero la ukosefu wa ajira walilosema ndilo linachangia vijana kufanya maandamano.

“Maandamano yaliyoshuhudiwa katika kaunti 27 kote nchini hayangeweza kufadhiliwa na Gachagua kwani yangemgharimu zaidi ya shilingi bilioni 10. Kwa hivyo, Rais Ruto na Waziri Murkomen wakubali kuwa vijana walijitokeza kwa hiari yao kutokana na changamoto zinazowakumba sasa, haswa ukosefu wa ajira,” akaeleza jana kwenye kikao na wanahabari katika majengo ya bunge.

Bw Mbui, ambaye ni mbunge wa Kathiani, alikuwa ameandamana na wenzake Jane Kihara (Naivasha), Wanjiku Muhia (Kipipiri), Augustine Kamande Mwafrika (Roysambu) na Seneta wa Murang’a Joe Nyutu.