Wabunge, Maseneta watofautiana kuhusu mgao wa bajeti
VUTA nikuvute imezuka kati ya Bunge la Kitaifa na Seneti kuhusu kiasi cha mgao wa bajeti kwa serikali za kaunti baada ya Bunge la Kitaifa kukataa pendekezo la Seneti kwamba serikali hizo ziongezewe Sh60 bilioni zaidi.
Wiki jana maseneta waliufanyia marekebisho Mswada wa Ugavi wa Fedha baina ya Serikali ya Kitaifa na Serikali za Kaunti wa 2025 (DORA) kwa kuongeza mgao wa fedha kwa kaunti kutoka Sh405 bilioni, ilivyoidhinishwa na wabunge hadi Sh465 bilioni katika mwaka ujao wa kifedha wa 2025/2026.
Mnamo Jumanne, Juni 3, 2025 kiongozi wa wengine katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah aliwaongoza wabunge kupinga hatua ya maseneta kuzingezea kaunti Sh60 bilioni akisema “Wizara ya Fedha haiwezi kumudu nyongeza hiyo.”
“Hatua ya maseneta kuufanyia marekebisho Mswada wa Ugavi wa Fedha kwa kuziongezea serikali za kaunti mgao wa fedha kutoka Sh405 bilioni hadi Sh465 bilioni haina mantiki yoyote. Hazina ya Kitaifa haiwezi kumudu nyongeza hiyo ya Sh60 bilioni na hivyo bunge hili linapinga nyongeza hiyo,” akasema Bw Ichung’wah ambaye ni Mbunge wa Kikuyu.
Akiunga mkono hatua hiyo, Mbunge wa Bumula Jack Wamboka alisema hamna haja kwa magavana kuongezewa mgao wa bajeti ilhali ubadhirifu wa pesa na ufisadi umekithiri katika kaunti zao.
“Badala ya bunge hilo kuongeza fedha za mgao wa bajeti kwa serikali za kaunti, pesa hizo zinapasa kuongezewa Hazina ya Maendeleo katika Maeneo Bunge (NG-CDF). Sababu ni maendeleo yaliyotekelezwa na fedha za hazina hii ndiyo huonekana katika kaunti zetu na wananchi walithibitisha walipotoa maoni ya kuhusu Mswada wa Marekebisho ya Katiba kuhusu uhalalishwaji wa NG-CDF,” akaeleza Mbunge huyo wa chama cha DAP-Kenya.
Kukataliwa kwa mapendekezo ya Seneti kuhusu ugavi wa fedha kwa serikali za kaunti sasa kunamaanisha kuwa Mswada wa Ugavi wa Fedha kati ya Serikali Kuu na Kaunti, 2025 utawasilisha kwa kamati ya maridhiano kutanzua suala hilo.
Kamati hiyo ya wanachama wanane itashirikisha maseneta wanne watakaoteuliwa na Spika wa Seneti Amason Kingi na wabunge wanne watakaoteuliwa na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula. Kamati hiyo inafanya vikao vya kutanzua mvutano huo.