Wabunge wachache wahudhuria sherehe ya waziri kusoma bajeti
IDADI ndogo ya wabunge walifika bungeni jana kumsikiza Waziri wa Fedha John Mbadi akisoma makadirio ya bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2025/2026, siku ambayo maandamano yalichacha jijini Nairobi.
Bw Mbadi alipokuwa akisoma bajeti hiyo, idadi kubwa ya viti katika ukumbi wa Bunge la Kitaifa vilisalia wazi, kinyume na miaka ya nyumba ambapo wabunge hujaa bungeni.
Duru ziliambia Taifa Leo kuwa wabunge wengi waliogopeshwa na maandamano hayo ya Gen Z, waliokuwa wakishikiza kujiuzulu kwa Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat.
Hii ni kutokana na mauaji ya mwanablogu Albert Ojwang’ kwa njia ya kutatatanisha katika kituo cha Polisi cha Central, Nairobi.
“Ni kweli kwamba baadhi ya wabunge walichelea kufika katika ukumbi wa bunge kwa hofu ya kukumbana na waandamanaji. Badala yake wameamua kufuatilia usomaji wa bajeti kwenye runinga zilizoko katika afisi zao za Jumba la Continental au tableti na simu za mkononi,” afisa mmoja wa bunge, aliyoamba tulibane jina lake, aliambia Taifa Leo.
Baadhi ya waandamanaji walijaribu kuteka barabara za Parliament Road na Harambee Avenue zinazutumiwa na wabunge kufika majengo ya Bunge.
Hata hivyo, polisi wa kupambana na fujo walikabiliana na waandamanaji hao kwa vitoa machozi na risasi kuwatawanya ili kutoa nafasi kwa Waziri Mbadi na wabunge kufika katika majengo ya Bunge.