Wafanyakazi wa INVESCO wakana ulaghai wa Sh309M
WAFANYAKAZI saba wa kampuni mbili za bima wameshtakiwa kwa ulaghai wa Sh309m.
Saba hao wameajiriwa kazi na kampuni za Invesco Assurance Company Limited na Compliant Insurance Agency Limited.
Maafisa watatu wakuu wa Invesco Albert Karakacha Muhavani (mkurugenzi), Daniel Wekesa Nalyanya (afisa mkuu masuala ya fedha) na Michael Ng’ang’a Kibara (mhasibu mkuu) walishtakiwa mbele ya hakimu mwandamizi mahakama ya Milimani Paul K Mutai mnamo Alhamisi Mei 29,2025.
Muhavani, Nalyanya na Kibara walikabiliwa na mashtaka mawili ya kula njama za kulaghai Sh309milioni za Invesco na kuekeza pesa hizo za Invesco Assurance kwa jina la kampuni nyingine (Compliant) katika akaunti ya Benki ya Oriental iliyoko katika jengo la Sameer.
Wafanyakazi wa Compliant walioshtakiwa ni pamoja na Ruth Wangari Mwasalu, Antony Githinji Ngerere, Hilda Wambui Karanja na Lameck Gesore.
Makampuni hayo ya Invesco na Compliant yalishtakiwa kwa kula njama kulaghai Sh309,207,570 zilizolipwa na wateja kutoka matawi 27 ya Invesco kote nchini.
Hakimu alielezwa washtakiwa hao walitekeleza uhalifu huo kati ya Aprili 13 na Agosti 13,2024.
Washtakiwa hao walikana shtaka a kuachiliwa kwa dhamana ya Sh300,000.
Kesi itatajwa baada ya wiki mbili kutengewa siku ya kusikizwa.