Habari

Wahuni wamvamia ajenti mkuu wa mwaniaji wa Upinzani kiti cha Evurore na kumjeruhi

Na GEORGE MUNENE February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MFUASI wa chama cha DP amejeruhiwa baada ya vurugu kuzuka katika uchaguzi mdogo wa kiti cha udiwani cha Evurore.

Kelvin Mwenda, ambaye ndiye ajenti mkuu wa mwaniaji wa DP Albert Kigoro alipata majeraha kichwani wakati wahuni walipomvamia akiwa katika kituo cha kupiga kura cha Njarage Primary.

Hofu ilitanda katika eneo hilo wakati ghasia zilipozuka katika kituo hicho cha kura.

Mwenda anadaiwa kupigwa huku akiendelea na shughuli zake katika kituo hicho. Anasemekana alikuwa akifanya kazi yake ya uangalizi wakati wahuni hao walipomvamia na kumpiga.

“Nilikuwa nafanya majukumu yangu ya uangalizi kama ajenti mkuu wa mwaniaji wa DP Albert Kigoro wakati kundi la wahuni liliponijia na kunipiga,” akahadithia.

Gari la Bw Kigoro pia liliharibiwa wakati wa uvamizi huo.

Kufuatia kisa hicho, Mwenda aliripoti katika kituo cha polisi cha Ishiara na kutaja tukio hilo kuwa la kumtishia maisha na kuvuruga kazi yake ya kuangalia utaratibu wa upigaji kura ulio huru na wa haki.

Alitaka vyombo vya usalama kukamata washukiwa na kuwafungulia mashtaka.