Habari

Waiguru: Sitastaafu hata muhula wangu ukiisha

Na GEORGE MUNENE June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Kirinyaga, Anne Waiguru, Alhamisi alitangaza kwamba hatastaafu siasa hata baada ya kukamilisha mihula yake miwili ya uongozi.

Waiguru kwa sasa anahudumu katika muhula wake wa pili na wa mwisho kama gavana.

“Siendi popote, bado nitakuwa kwenye siasa,” alisema.

Bi Waiguru alidokeza kuwa analenga wadhifa wa juu zaidi baada ya kumaliza muda wake kama Gavana.

Wakati huo huo, Gavana alithibitisha kujitolea kwake katika kutengeneza sera faafu kwa biashara ili kuvutia uwekezaji zaidi wa viwanda katika kaunti hiyo.

Alisema kuwa Kaunti hiyo imepiga hatua kubwa kuelekea mageuzi ya kiuchumi huku viwanda vya kuongeza thamani ya mazao vikifunguliwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa kiwanda cha kusaga unga cha Nice Extra Premium Flour Milling cha thamani ya mamilioni ya pesa huko Ngurubani, Waiguru alisema serikali yake imeunda mazingira bora kwa biashara kustawi.

“Kirinyaga ni eneo mpya la uwekezaji kutokana na mazingira tuliyoyaweka. Huna haja ya kumjua mtu yeyote ili uweze kuanzisha biashara Kirinyaga,” alisema Waiguru.

Aliongeza kuwa mbali na kuwekeza katika miundombinu bora, kisasa na sera bora kwa biashara, upatikanaji wa malighafi kwa uzalishaji unawavutia wawekezaji kuja Kirinyaga.