Wakazi wabuni mbinu za kukabiliana na joto msimu huu wa kiangazi
WAKAZI wa Turkana sasa wanabuni mbinu mbalimbali za kukabiliana na joto kali msimu huu.
Kwa baadhi ya Wakenya, hali hii ya joto si suala la kero tu bali ni changamoto kubwa kiafya na kiuchumi.
Emmanuel Kagiri, dereva wa teksi jijini Nairobi, amelazimika kupanga maisha yake kulingana na mzunguko wa jua.
“Ni mateso kufanya kazi mchana kukiwa na joto kali,” anasema. “Napata maumivu ya kichwa mara kwa mara na ngozi yangu huwa inawasha na kuungua.”
Alipotafuta matibabu, daktari alimweleza kuwa uchovu wake ulitokana na kukosa usingizi wa kutosha. “Hata hivyo, najua huwa ninalala mapema,” anasema.
Ilikuwa baada ya safari yake Botswana, ambako alikumbwa na wimbi la joto, ndipo daktari mwingine alipohusisha hali yake na athari za joto kali.
Sasa amezoea ratiba mpya: “Ninaamka mapema, nafanya kazi hadi saa tano asubuhi, halafu narudi kufanya kazi usiku.”
Kwa wafanyakazi wa nje, joto ni changamoto isiyoweza kuepukika.
Fredrick Mureithi, dereva wa bodaboda jijini Nairobi, bado huvaa koti lake zito licha ya jua kali, lakini macho yake ndiyo huathirika zaidi.
“Nikivaa helmeti kwa usalama, mwanga wa jua huwaka kwenye kioo cha helmeti na kuathiri macho,” anaeleza. “Ninalazimika kufungua kioo hicho, ambacho huzuia vumbi, na inakuwa vigumu kuendesha bila helmeti.”
Joto pia linaathiri biashara yake.
“Tunatokwa jasho sana. Tofauti na siku za baridi, lazima tubadilishe makoti kila siku ili wateja wahisi vizuri. Tusipofanya hivyo, tunapoteza wateja.”
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa nchini (KMD), Edward Muriuki, anaeleza kuwa viwango vya sasa vya joto bado viko ndani ya kiwango cha kawaida cha msimu wa Januari, ambao kihistoria ni miongoni mwa miezi yenye joto kali zaidi nchini.
Nairobi kwa kawaida hupata joto la kati ya nyuzi 26 hadi 28 Selsiasi kati ya Januari na Machi, ingawa nyakati zingine joto limewahi kupanda zaidi. Mnamo Machi 2019, joto lilifikia nyuzi 30.
“Ingawa baadhi ya maeneo yanapitia joto la juu kidogo kuliko wastani, hali hii ilitabiriwa mapema na KMD,” anasema Muriuki.
“Hisia za kuwa joto ni la kipekee zinatokana pia na uelewa mkubwa wa umma, taarifa nyingi, na mabadiliko ya muda mrefu ya hali ya hewa.”
Anafafanua kuwa wimbi la joto hutangazwa pale halijoto inapozidi viwango maalum vya eneo fulani kwa siku kadhaa mfululizo na kuhatarisha afya, maisha na miundombinu.
Kulingana na utafiti wa KMD, wimbi la joto Nairobi ni pale joto linapozidi nyuzi 32 kwa siku mbili mfululizo.
“Hali ya sasa ni ya joto na inaweza kusababisha usumbufu, lakini bado haijavuka viwango hatari kwa muda mrefu,” anasema.
Maeneo ya Pwani, Kaskazini Mashariki, Kaskazini Magharibi na nyanda za chini za Kusini Mashariki yanaongoza kwa viwango vya juu vya joto, kutokana na ukame.
Maeneo ya ndani kama Bonde la Ufa na Bonde la Ziwa Victoria pia ni ya joto, huku maeneo ya miinuko yakibaki baridi zaidi hasa usiku.
Kaunti ya Turkana inakumbwa na joto kali zaidi.
Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri wa Hali ya Hewa kaunti hiyo, Francis Muinda, anasema joto limekuwa kati ya nyuzi 36 na 37 Selsiasi mwezi huu, na linatarajiwa kufikia nyuzi 40 hadi 41 mwishoni mwa Februari.
“Tutafikia kilele Machi 22, 2026, jua litakapokuwa juu moja kwa moja kwenye ikweta,” anasema.
Anashauri wakazi kunywa maji mengi, kuepuka jua kali na kukaa kwenye kivuli. Wachungaji wanashauriwa kubeba maji wanapochunga mifugo na kulala nje ya manyatta usiku kwani nje huwa baridi zaidi.
Afisa Mkuu wa Huduma za Afya Turkana, Dkt Gilchrist Lokoel, anaonya kuwa joto kali linaweza kusababisha kiharusi cha joto na mawe ya figo endapo watu hawatakunywa maji ya kutosha.
Katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Lodwar, Mkurugenzi Mtendaji Nancy Kinyonge anasema wagonjwa wanaoathiriwa na upungufu mkali wa maji na uharibifu wa figo wameongezeka. “Kwa sasa tuna wagonjwa 28 wa figo, asilimia 60 wao ni vijana,” anasema
.
Katika maeneo ya mbali Turkana, wafugaji hubeba maji kwenye chupa zilizofungwa kwa vitambaa au magunia ili kuyaweka baridi.
Katika maeneo ya mbali Turkana, wafugaji hubeba maji kwenye chupa zilizofungwa kwa vitambaa au magunia ili kuyaweka baridi.