Wakenya kulipa Sh3bn kwa ziara za Ruto nje ya nchi kutoka sasa hadi Juni 30
WALIPA Ushuru wanatarajiwa kutoa Sh3.1 bilioni kufadhili ziara za Rais William Ruto nje ya nchi, ikiwa imesalia miezi miwili pekee kabla ya kutamatika kwa mwaka huu wa kifedha.
Stakabadhi ambazo zimewasilishwa bungeni zinaonyesha kuwa Wizara ya Masuala ya Kigeni imeamrishwa ifadhili ziara 11 za Rais Ruto kati ya sasa hadi Juni 30, 2026 kwa kima cha Sh3.1 bilioni.
Katibu katika Wizara ya Masuala ya Kigeni Korir Sing’oei aliambia Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi, Ujasusi na Uhusiano wa Kigeni kuwa wizara hiyo tayari imetumia Sh2.2 bilioni kati ya Sh1.8 bilioni ambazo ilitengewa katika bajeti ya 2025/26 kwa ziara za nje.
“Pia idara hii imeamrishwa ijiandae na kufadhili ziara 11 zaidi ya nje kufikia Juni 2026 kwa kima cha Sh3.1 bilioni,” akasema Dkt Singóei.
Alisema hayo mbele ya kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Belgut Nelson Koech huku akitetea mgao waliotengewa kwenye bajeti ya ziada ya 2025/26.
Alisema ziara zote za serikali zinahitaji Sh5.3 bilioni na Sh2.2 bilioni walizotengewa hazitoshi kukiwa bado kuna mwanya wa Sh3.5 bilioni.
“Suala hili linahitaji kuingiliwa ili upungufu huu uondolewe na ziara za Rais ziendelee,” akaongeza Dkt Singóei.
Ikulu iliwasilisha ripoti Bungeni iliyoonyesha kuwa kati ya Oktoba 31, 2024 hadi Septemba 22, 2025, rais alifanya ziara 24 za kikanda na nje ya nchi.
Katika kipindi hicho alikuwa mwenyeji wa marais 10, ambao watano walifika kwa ziara rasmi za serikali.
Ziara za nje mnamo 2024/25 zilikuwa za chini ya 31 ambazo Rais alifanya kati ya Julai 2023 na June 2024. Kati ya Julai 2022 na Juni 2024, Rais alizuru nchi 28.
Na kati ya ziara hizo 31 mnamo 2023/24, ni tisa pekee ambazo zilikuwa rasmi za serikali huku nyingine zikiwa za makongamano, vikao na za kibinafsi.
Mnamo 2024, Rais Ruto alitoa amri ya kuzuia safari nyingi za nje zisizokuwa na umuhimu baada ya maandamano ya Gen Z ya kulalamikia ushuru mwingi uliokwepo kwenye Mswada wa Fedha 2024.
Wakati huo huo, Mdhibiti wa Bajeti ya Serikali ameanika ubadhirifu ambao umekuwa ukiendelezwa na serikali licha ya ahadi za kuzima matumizi ya kiholela.
Katika ripoti ambayo imeshughulikia miezi sita katika mwaka huu wa kifedha, Dkt Nyakangó alifichua kuwa afisi ya rais ilitumia Sh768.5 milioni kwenye safari za ndani na Sh1.165 bilioni kwa safari za nje.