Wakenya watekwa na uraibu wa kamari kupitia mchezo wa Aviator
JIONI moja mnamo Desemba mwaka jana, Mwas* aliketi na kuwaandikia wazazi wake barua ya kuaga dunia.
Alikuwa ametumbukia kwenye uraibu wa kamari kupitia mchezo wa Aviator, mojawapo ya michezo maarufu zaidi ya kubashiri nchini Kenya kwa sasa.
“Aviator inaniteka kabisa. Nimezama ndani yake na siwezi hata kujadiliana nanyi, imeniharibia kila kitu na sina njia ya kutoka,” aliandika.
Aviator ni mchezo wa kubashiri ambapo mchezaji hulazimika kutoa dau lake kabla ya ndege ya mtandaoni “kuruka”.
Kadri ndege inavyokaa hewani ndivyo faida inavyoongezeka, lakini ikiondoka kabla ya kutoa dau, mchezaji hupoteza kila kitu.
Kwa Mwas, aliyekuwa anapambana kujiondoa kwenye uraibu huo, ahadi ya kupata pesa haraka ilimvutia sana.
Alichukulia kama burudani mwanzoni, lakini baadaye ikawa uraibu uliomsukuma kwenye madeni makubwa.
Alianza kucheza usiku kucha, akiweka dau mara kwa mara na kutumia maelfu ya pesa. Tatizo lake lilichangiwa pia na matumizi ya pombe.
Wiki tatu kabla ya kuandika barua hiyo, alimkabidhi mpenzi wake simu baada ya mabishano makali kuhusu fedha.
Tulikutana naye katika Kituo cha Urekebishaji tabia cha Resolutions Recovery Centre, ambapo alikuwa amejisajili mwenyewe kupata msaada.
Mwas ni miongoni mwa maelfu ya vijana nchini wanaokumbwa na uraibu wa kamari.
Wataalamu wanasema uraibu huu huanza polepole lakini huweza kuharibu maisha, mahusiano na afya ya akili.
Mshauri wa uraibu Chrispus Githae Kimaru anasema wengi huanza kamari wakitafuta fedha za matumizi ya kila siku au kulipa madeni.
“Sio njia endelevu, lakini wengi hawajui,” anasema.
Mwas anakiri kuwa alishawishiwa na marafiki alipokuwa chuoni.
“Nilitaka tu pesa za kujifurahisha na marafiki na kununua vitu walivyokuwa navyo,” alisema.
Alipoteza hadi Sh40,000 zilizokuwa za biashara ya wazazi wake.
Hata baada ya wazazi wake kumpeleka kwa ushauri na kumpokonya simu, aliendelea kubeti kwa siri.
Mshauri mwingine, Harrison Irungu, ambaye pia aliwahi kuwa mraibu wa kamari, anasema uraibu huu ni rahisi kuficha.
“Mtu anaweza kuweka dau la Sh100,000 mara moja na usijue,” anasema.
Irungu alipoteza kazi, ndoa na fedha nyingi kutokana na kamari.
Alianza kubeti akitafuta pesa zaidi za familia lakini akaishia kuiba fedha kazini.
Hatimaye alifukuzwa kazi na ndoa yake kuvunjika.
Anasema mabadiliko yalikuja baada ya kukubali tatizo na kurejea kituo cha urekebishaji.
Baadaye alisomea ushauri wa kisaikolojia na sasa ni mshauri wa uraibu.
Dkt Linus Oyugi wa Chiromo Hospital Group anasema uraibu wa kamari huathiri ubongo kama vile dawa za kulevya.
Wataalamu wanaonya kuwa vijana wako hatarini zaidi kwani sehemu ya ubongo inayodhibiti maamuzi bado haijakomaa kikamilifu.
Ingawa si kila mtu anayebeti huwa mraibu, mazingira, hulka na marafiki vina mchango mkubwa.
Shirika la Waendeshaji Michezo ya Kamari Kenya (AGOK) linasisitiza umuhimu wa kubeti kwa uwajibikaji na kuzingatia mipaka.
Hata hivyo, hadithi za Mwas na Irungu zinaonyesha kuwa kwa wengi, kamari si burudani bali mtego hatari unaoweza kuharibu maisha.
Wataalamu wanaonya kuwa athari za uraibu wa kamari kama Aviator zinaweza kuwa za muda mrefu na zenye madhara makubwa kwa jamii.
Wanasema mbali na kupoteza fedha, waathiriwa hupoteza mwelekeo wa maisha, kuharibu mahusiano ya kifamilia na hata kupoteza ajira.
Wazazi na walezi pia wametakiwa kuwa makini na mienendo ya vijana wao, hasa kutokana na urahisi wa kufikia michezo ya kamari kupitia simu za mkononi.
Dalili kama kukosa usingizi, matumizi ya fedha kupita kiasi na kujitenga na familia zinaweza kuwa ishara za awali za uraibu.
Serikali na wadau katika sekta ya michezo ya kubahatisha pia wamehimizwa kuimarisha udhibiti na kampeni za uhamasishaji ili kupunguza madhara ya uraibu huo.
Wataalamu wanasisitiza kuwa msaada wa kitaalamu, ikiwa ni pamoja na ushauri nasaha na vikundi vya kujisaidia, unaweza kusaidia waathiriwa kurejea katika maisha ya kawaida.
Kwa wengi kama Mwas, safari ya kupona ni ndefu, lakini inawezekana kwa msaada sahihi na uamuzi thabiti wa kubadilika.